Somo la mwezi mmoja Russia lionekane kwa vitendo sasa

Muktasari:

  • Mataifa ya Ufaransa na Croastia yalitambuka kwa kuruka viunzi vyote na kuingia fainali.

Fainali za Kombe la Dunia 2018 zimefikia ukingoni na jana Jumapili ndio zilifikia tamati baada ya mwezi mmoja wa hekaheka kule Russia.

Mataifa ya Ufaransa na Croastia yalitambuka kwa kuruka viunzi vyote na kuingia fainali.

Wachezaji wa mataifa hayo, hawakuwa na kazi nyepesi ikizingatiwa kuwa mataifa 30 hayakuwa mepesi, kwani kila moja alijiandaa kikamilifu akiamini kuwa mechi zitakuwa ngumu.

Wakati fainali zikimalizika, ninaamini kuna mengi ambayo wadau hao wa soka wakiwamo wachezaji, makocha, waamuzi, viongozi wa soka na hata mashabiki na wanachama wa klabu zetu, watakuwa wamejifunza.

Pamoja na kuwepo na kasoro za hapa na pale, lakini ninaamini kwa yeyote aliyefuatilia kwa karibu fainali tangu mechi ya ufunguzi atakuwa amepata somo la kutosha.

Kwa makocha, waamuzi na hata wachezaji ninatarajia kuona kwenye msimu mpya wa Ligi Kuu Bara 2018-2019.

Tutayaona kivipi? Ni kwa kuona ligi hizo na mwenendo mzima wa timu zetu kupitia wachezaji waliofuatilia fainali za hizo za Russia, wakiyahamishia kwenye viwanja vyetu.

Kwa makocha, kuna utaalamu ambao umeonekana. Mbinu za kujenga mashambulizi kuanzia katika ngome, viungo hadi washambuliaji.

Mbinu za kupiga kona, mipira iliyokufa na kutumia nafasi ama ndani ya 18 au nje kidogo ya 18.

Tumeshuhudia wachezaji wakipiga mashuti makali yaliyonyoona na kujaa wavuni, sasa kwa wachezaji wetu washambuliaji, si lazima kufika langoni na kufunga, kutumia eneo la 18 vizuri.

Wakati mwingine inashangaza kuona wachezaji wanashindwa hata mipira iliyokufa.

Nikiwaangalia waamuzi. Hapa ni utata ninaweza kusema. Suala la VAR lilibeba sura ya mechi za Kombe la Dunia, lakini kwa mtazamo wa mbali na karibu, hazina maana sana kwa kuwa ni kama zililetwa kisiasa.

Mfano, ninasema hazima naama kwa maana ipi, wakati fulani zinatumika sawasawa, lakini linapokuja suala la mwamuzi kuwa na mamlaka juu ya VAR, hapo ndipo inapotia ikakasi.

Niliwahi kuandika hapa kwamba mwamuzi asiyekuwa mwadilifu haiwezi VAR kwa maana ya kwamba VAR inatumika lakini bado uamuzi wa mwisho ni mwamuzi mwenyewe. Ndiyo maana Nigeria ililalamikia, Brazil ililalamikia, Senegal kadhalika walilalamikia VAR.

Fifa inasema kuwa VAR ipo lakini bado mwamuzi ataamua kulingana na vile anaona aamue vipi, iwe hata baada ya kujiridhisha baada ya kuangalia VAR. Haijatulia kabisa hii.

Kadhalika hata kwa waamuzi, tunaamini kuna mengi zaidi wamejifunza kupitia fainali hizi za Kombe la Dunia kama wachezaji kujilaza, rafu za kizembe pamoja na nguvu za wachezaji.

Yapo mengine yaliyofanywa na waamuzi katika kuchezesha kwa ufanisi na kutoa uamuzi sahihi kwa muda sahihi, kiasi cha kufanya timu zilizopoteza kutoka uwanjani zikiwa zimeridhika kwanini waamuzi wetu wasiige?

Mazuri yaliyojiri katika fainali za Kombe la Dunia ni mengi, hata kama yapo mengi ya ovyo yaliyoibuka huko, lengo ni kuona soka letu linasonga mbele ni vyema kuiga yale ya maana na kuwaachia wenyewe yale ya ovyo.

Wadau wa soka lazima wajue kuwa lazima kubadilika na kuonyesha walikuwa darasa kwa mwezi mzima.

Waamuzi wakisimamia kilichojiri Russia ukiondoa VAR ninaamini watapata sifa na si vinginevyo.