VIDEO: Maria na Consolata walipishana dakika 10 kuaga dunia

MWANZO MWISHO WA MARIA NA CONSOLATA

Muktasari:

  • Daktari asema Maria ndio alianza kufariki, Consolata alimueleza daktari kuwa wanakufa na baada ya muda naye aliaga dunia

Iringa. Mganga Mkuu mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Iringa, Museleta Nyakiloto amezungumzia vifo vya pacha walioungana Maria na Consolata Mwakikuti, akieleza kuwa walipishana dakika 10 kufariki dunia.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumapili Juni 3, 2018, Nyakiloto amesema walifariki dunia jana saa 2 usiku katika hospitali ya mkoa wa Iringa walikokuwa wakipatiwa matibabu.

“Walikuwa na tatizo la upumuaji. Walipishana dakika 10 kuaga dunia wakati wakipatiwa matibabu ICU (chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum). Walikuwa wamelazwa tangu Mei 17, 2018 walipotoka Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dar es Salaam,” amesema.

 “Tangu wafike hospitalini hapa hatukuwahi kuona wamebadilika kiasi kile. Maria ndio alitangulia kufariki na baada ya dakika kumi alifuata Consolata. Consolata alipomuona Maria anahangaika na umauti kumkuta naye alihangaika na kumwambia daktari kuwa wanakufa, baada ya muda na yeye aliaga dunia.”