Mmoja afariki ajali ya gari la wagonjwa la JWTZ

Kamanda wa Polisi Pwani Wankyo Nyigesa akitoa taarifa ya ajali ya gari la wagonjwa mali ya jeshi la wananchi JWTZ (inayoonekana pichani) iliyogonga gari jingine eneo la Kibiki Chalinze agosti 31 na kusababisha kifo cha mtu mmoja na majeruhi wanne , kulia ni mkuu wa wilaya ya kipolisi  Chalinze (OCD)  Janeth Magomi na mkuu wa kikosi cha usalama barabarani (RTO) Pwani Mosi Ndozero

Muktasari:

  • Gari hilo lilikuwa likisafirisha mgonjwa kutoka Dodoma kuelekea Dar es Salaam

Chalinze. Mtu mmoja amefariki dunia na wanne kujeruhiwa baada ya gari la kubeba wagonjwa la Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kuligonga gari jingine kwa nyuma katika eneo la Kibiki kata ya Bwilingu halmashauri ya Chalinze mkoani Pwani.

Akizungumza leo Ijumaa Agosti 31, 2018 Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, Wankyo Nyigesa amesema ajali hiyo imetokea leo ikihusisha gari hilo la wagonjwa la kikosi cha 911KJ cha Ihumwa, Dodoma.

Amesema gari hilo lilikuwa linasafirisha mgonjwa kutoka mkoani Dodoma kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), jijini Dar es Salaam.

Amemtaja aliyefariki dunia kuwa ni Elinikunda Mushi (50) ambaye alikuwa mgonjwa, kwamba alikuwa amekwenda Ihumwa kwa mwanae, Ufo Swai.

“Hili gari la JWTZ lilikua linaendeshwa na askari Shabani Mpwate, lilipofika eneo la  Kibiki dereva aliligonga gari jingine aina ya Toyota Canter kwa nyuma, Canter hilo lilikuwa limeegeshwa kando ya barabara kwa matengenezo,” amesema.

Amewataja majeruhi katika ajali hiyo kuwa ni Beatrice Shidodolo ambaye ni muuguzi wa Hospitali ya Mkoa wa Dodoma, dereva wa gari lililogongwa,  Justine Patrick na fundi wa gari hilo, Rashid Rais pamoja na Swai.

Amesema katika uchunguzi wa awali wamebaini kuwa katika gari hilo la wagonjwa pia kulikuwa na watu wengine wanne ambao hawakupata majeraha yoyote.

Amesema abiria hao ni askari  MT 3480 SGT Elimasa Mushi,  MT 95881 PTE Taulin Karia,  Eveline Stanley (25) na mtoto mwenye umri wa miezi 11, Nicholous Petro.

Amebainisha kuwa mwili wa marehemu umehifadhiwa katika  hospitali ya Jeshi Lugalo jijini Dar es Salaam huku majeruhi pia wakipata matibabu katika hospitali hiyo.

“Dereva wa gari la JWTZ tunamshikilia kwa mahojiano na uchunguzi  kwa sababu hata kama ni gari la wagonjwa lazima tujiridhishe na sisi,” amesema.