Hisa Vodacom zarejea bei ya awali

Muktasari:

Bei hiyo imeongezeka kwa Sh110, baada ya kupungua hadi Sh740 mwishoni mwa wiki iliyopita

Dar es Salaam. Bei ya hisa za kampuni ya simu ya mkononi ya Vodacom Tanzania imerejea kwenye kiwango chake cha awali cha Sh850.

Taarifa ya soko la hisa imeonyesha kwamba, bei hiyo imeongezeka kwa shilingi Sh110, baada ya kupungua hadi Sh740 mwishoni mwa wiki iliyopita.

Ripoti ya mauzo ya hisa ya jana Januari 29, mwaka 2018 imeonyesha kwamba bei ya hisa za kampuni hiyo zilirejea kwenye bei ya Sh850, ambacho ni sawa na kiwango cha bei ya mauzo ya hisa za awali (IPO).

Ripoti ya soko imeonyesha kwamba kampuni hiyo ilirekodi mauzo ya Sh21.6 milioni baada ya mauzo ya hisa 29,590 zilizouzwa kwa bei ya juu ya Sh730 kwa mikupuo 13.

Ongezeko la bei ya hisa pia limesababisha kuongezeka kwa mtaji wa jumla hadi Sh1.9 trilioni kutoka Sh1.6 trilioni zilizorekodiwa mwishoni mwa wiki iliyopita.

Hata hivyo, wawekezaji wanaouza hisa zao kipindi hiki, wanauza kwa bei ya hasara kwani bei ya kuuzia ilikuwa Sh730 Jumatatu.

Wachambuzi wa masoko ya mitaji wanasema bado kuna uwezekano wa bei ya hisa za kampuni hiyo kuongezeka zaidi baadaye kwani ina muda mfupi tangu kuorodheshwa.