Mtoto atumbukia mtoni, afariki

Muktasari:

Mwenyekiti wa kitongoji hicho, Bahati Nyalile alisema tukio hilo lilitokea jana mchana Septemba 3,2018 wakati mtoto huyo akiwa na wenzake wawili wakiwa wametoka shuleni wanakosoma Shule ya Msingi Mlima Reli walifika mtoni hapo kwa ajili ya kuoga ndipo akatumbukia.

Mbeya.  Mtoto Christopher Michael (10) mkazi wa Kitongoji cha Tunduma Roada, Kata ya Nsalala Wilaya ya Mbeya, ameafariki baada ya kutumbukia kwenye Mto Mbalizi wakati akicheza na wenzake.

Mwenyekiti wa kitongoji hicho, Bahati Nyalile alisema tukio hilo lilitokea jana mchana Septemba 3,2018 wakati mtoto huyo akiwa na wenzake wawili wakiwa wametoka shuleni wanakosoma Shule ya Msingi Mlima Reli walifika mtoni hapo kwa ajili ya kuoga ndipo akatumbukia.

Alisema baada ya kutumbukia watoto wenzake walitoa taarifa kwa mwanamke mmoja aliyekuwa karibu akifua nguo zake, ndipo wakaenda kutoa taarifa nyumbani kwa wazazi na kwa wananchi na watu wakakusanyika kwa ajili ya kumtafuta bila mafanikio.

“Jana tulilazimika kufunga mto huo ili maji yapungue kwenye korongo lile ambako maji hujirusha pale lakini shughuli hiyo ikawa ngumu na wengine wamekesha hapa bila mafanikio na le alfajiri tumekusanyika tena hapa kwa kazi ya kumtafuta na tushukuru tumempata, na akiwa amevaa nguo zake za shule,” alisema Nyalile.

Diwani wa Nsalala, Kissman Mwangomale alisema ‘Hili eneo ni hatari sana na watoto wanapenda sana kuja kuoga hapa.”

“Na hili ni tukio la pili huku nyuma iliwahitokea watoto wawili walizama maji hapa hapa. Hivyo tunachokiona hapa ni kuiomba Serikali itusaidia kuja kupiga barti ili kupasua mwamba huu maana ni mwamba mgumu ambao umetengeneza kama korongo hivi ili tuweze kutengeneza ‘Level’ moja.”

Alisema, “Au itupe ridhaa sisi wananchi Serikali ituruhusu tuifanye kazi hii, maana vinginevyo tutaendelea kupoteza watoto na ikizungatiwa hata kama  tutaweka ulinzi lakini sio muda wote kutakuwa na mtu anayeshinda hapa.”

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ulrich Matei  alisema wanaendelea na uchunguzi zaidi wa tukio hilo huku akitoa wito kwa wazazi kuendelea kuwa karibu na watoto muda wote.

“Ni kweli tukio hilo limetokea mtoto huyo akiwa na wenzake wawili walifika eneo la mto huo Mbalizi na bahati mbaya akatumbukia. Na baada ya kuona hivyo wenzake walitoa taarifa kwa wananchi na juhudi za kumuokoa zilianza mara moja lakini kwa juzi ile walishindwa kumpata na jana asubuhi baada ya maji kupungua ndio wamemkuta akiwa ameshafariki tayari”.