Nape alivyojitabiria kuvuliwa uwaziri wa habari

Muktasari:

Mara nyingi mambo au kauli hizo huonyesha kama vile alikuwa akiona tukio likimjia au kumtokea.

Dar/Mikoani. Mtu anapopatwa na jambo, ni kawaida ya binadamu kuangalia mambo au kauli zake alizokuwa akitoa kabla ya kufikwa na tukio hilo.

Mara nyingi mambo au kauli hizo huonyesha kama vile alikuwa akiona tukio likimjia au kumtokea.

Unaporejea kauli za hivi karibuni za Nape Nnauye, unaona dhahiri kuwa alikuwa kama anaona kinachokuja na kujitabiria kuwa angevuliwa uwaziri wa habari, utamaduni, sanaa na michezo.

Kauli ya mwisho na yenye nguvu aliitoa juzi mchana wakati wa mkutano na waandishi wa habari wa kukabidhiwa ripoti ya uchunguzi kuhusu tukio la uvamizi wa studio za televisheni za kampuni ya Clouds Media Group.

“Niseme tu kwamba nimepokea ripoti na kama nilivyosema kazi hii si rahisi sana, ina gharama kubwa sana. Gharama ya kusimamia haki, kusimamia ukweli,” alisema juzi.

Kauli hiyo aliirudia jana wakati akiongea na waandishi wa habari nje ya Hoteli ya Protea baada ya kuzuiwa kufanya mkutano wake ndani.

Nape aliondolewa katika nafasi hiyo katika mabadiliko madogo yaliyofanyika jana asubuhi, siku moja baada ya kukabidhiwa ripoti hiyo ambayo aliahidi angeiwasilisha kwa mamlaka za juu, ambazo alizitaja kuwa ni Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Rais.

Katika mabadiliko hayo, Rais Magufuli amemteua Profesa Palamagamba Kabudi kuwa Waziri wa Katiba na Sheria, nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Dk Harrison Mwakyembe ambaye anaziba nafasi ya Nape.

Ni kama Nape alikuwa akiona gharama za kusimamia haki za Clouds Media za kutoingiliwa katika shughuli zake na viongozi baada ya kituo hicho kuvamiwa na askari waliokuwa na silaha za moto wakimsindikiza kiongozi aliyekwenda kuhoji sababu za kituo hicho kutorusha habari ya ‘umbea’ iliyokosa sifa stahiki.

Maneno hayo ya Nape ni sehemu ya mlolongo wa kauli za utabiri ambazo amekuwa akizitoa kwa siku chache zilizopita wakati akizungumza na waandishi na kwenye mitandao ya kijamii.

Baada ya kituo cha Clouds kuvamiwa, Nape alituma ujumbe kwenye akaunti yake ya Tweeter Machi 20 akisema “No Longer at Ease”, ikiwa ni nukuu ya kitabu cha fasihi kilichoandikwa na Chinua Achebe mwaka 1960 kumaanisha hakuna marefu yasiyokuwa na mwisho.

Siku hiyo, Nape alituma ujumbe mwingine katika akaunti hiyo akisema “each day is a day of decisions, and our decisions determin our destiny” akimaanisha “kila siku ni siku ya uamuzi na uamuzi wetu huamua mustakabali wetu”.

Kama vile haitoshi, Nape alituma ujumbe mwingine siku hiyo akisema “majaribu huja ili kutuinua kutoka utukufu hadi utukufu. Kikubwa tusikate tamaa, utukufu mkubwa upo mbele. Quaresma njema”.

Nape aliandika hayo wakati mchakato wa kamati aliyoiunda ikiendelea kuchunguza tukio la Clouds kuvamiwa.

Na alikuwa na ushauri kwa wanasiasa wengine. “Na kwa kuwa sisi wengine tuliopewa dhamana ya kuwatumikia watu ni vizuri kujifunza kuwa wanyenyekevu, kwanza ina baraka kwa Mwenyezi Mungu, lakini pia tutakuwa tunawatendea haki Watanzania ambao ndiyo wametuchagua na kutuweka kwenye madaraka.”

Baada ya kuvuliwa uwaziri, Nape jana alituma tena ujumbe katika akaunti yake ya Tweeter akiandika kwa herufi kubwa baadhi ya maneno kuweka msisitizo.

“Ndugu zangu naomba TUTULIE! LEO (jana) mchana nitakutana na wanahabari na tutalizungumza hili. Nitawaambia saa na mahali. Kwa sasa naomba TUTULIE!”

Baadaye akatuma ujumbe mwingine akisema “tukutane saa nane kamili Protea Hotel karibu na St. Peter. Nitakutana na wanahabari. Karibuni sana!”

Kauli za wadau

Wadau wa habari wakiwamo wanasiasa, wasomi, wachambuzi wa masuala ya kisiasa na wanahabari wameeleza kushtushwa na mabadiliko hayo na kummimia sifa mbunge huyo wa Mtama.

Katibu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Nevile Meena alisema tasnia ya habari imepokea kwa huzuni taarifa hiyo, hasa kutokana na ukweli kuwa ameondoka katika kipindi ambacho alikuwa karibu na wadau akitetea uhuru wa habari.

“Tulitegemea Nape angeondoka wizara hiyo, lakini hatukutegemea ingekuwa kwa mtindo huu. Katika sakata hili Nape alionyesha wazi kutoegemea upande wa Serikali na alisimamia haki,” alisema Meena.

Kuhusu nafasi hiyo kuchukuliwa na Dk Mwakyembe, Meena alisema tasnia inamkaribisha, ikitegemea atafanya vizuri, “asipokwenda sawa tutaenda naye hivyohivyo”.

Kauli ya masikitiko pia ilitolewa na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari (UTPC) ambayo rais wake, Deogratius Nsokolo alisema, “Nape alikuwa karibu mno na waandishi na wadau wote wa habari na alikuwa akisimamia haki”.

Alisema huenda kilichomgharimu Nape ni kwenda kutembelea kituo cha Clouds na kuunda kamati ya kuchunguza uvamizi huo.

“Nimsihi Nape asikate tamaa. Yeye ni mwanasiasa mzuri na mkomavu. Hakuna ubishi tena, ni shujaa ambaye amejitoa kusimamia haki. Sina uhakika sana kama atakayeshika nafasi yake atakuwa kama yeye,” alisema.

Wanasiasa

Akizungumzia kuondoka kwa Nape, Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe alisema haitoshi kumlilia Nape, bali wananchi wanapaswa kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria.

“Haifai tu kumlilia Nape kwamba anaonewa, tunapaswa kumuwajibisha Rais ambaye amechaguliwa na wananchi. Anapaswa kuwa mnyenyekevu kwa wananchi na hatupaswi kuendekeza tabia zozote za utawala wa kiimla,” alisema kiongozi huyo wa ACT Wazalendo.

“Ni lazima sisi viongozi tuwaelekeze wananchi mabaya au mazuri na tuwaelekeze kuchukua hatua.”

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema kilichotokea ni uthibitisho wa madai ya muda mrefu ya wapinzani kuwa Rais Magufuli anapingana na mawazo ya wananchi wake.

“Huu ni uthibitisho kuwa tuna Rais ambaye anapingana na maoni ya watu anaowaongoza. Kinachoendelea hapa si Rais au Nape, bali ni hisia za wananchi. Nape amejipambanua hivi karibuni kama waziri makini na alichokifanya kiko ndani ya uwezo wake,” alisema Mbowe.

“Sisi kama wapinzani tunaona tunashamiri kwa sababu CCM inasambaratika, lakini si jambo la kufurahi tu, bali tuisaidie nchi yetu.

“Kitu cha msingi Rais anapaswa kuwa mwepesi wa kusikiliza kuliko kuongea. Marais wengi wamefanikiwa kwa kusikiliza wananchi wao, lakini Rais Magufuli ni tofauti, anaongea kuliko kusikiliza maoni ya wananchi wake. Ndiyo maana mawaziri wanajiuzulu, wabunge wanajiuzulu kwenye kamati zao, yote kwa sababu Rais hataki kusikiliza maoni yao,” alidai Mbowe.

Lakini Mkurugenzi wa Taasisi ya Demokrasia na Utawala Bora (Fordia), Bubelwa Kaiza aliunga mkono hatua ya Rais Magufuli akisema kuwa aliitarajia.

“Binafsi hatua hii niliitegemea kwa sababu vitendo alivyovifanya Nape ni kama hakujua kuwa Serikali ndiyo inayojisimamia. Alipaswa kuomba ushauri kabla ya kuunda ile kamati yake,” alisema Kaiza.

“Ni kweli kama Waziri wa Habari angekwenda kutembelea Clouds Media, lakini asingesema chochote. Lakini yeye aliunda kamati na kufanya aliyofanya jana (juzi). Kwa Serikali iliyo makini ni lazima izibe vaccum (ombwe) inayojitokeza.”

Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), Francis Nanai alisema kama wamiliki wa vyombo vya habari wako tayari kufanya kazi na waziri yeyote anayeteuliwa na Rais, ilimradi tu afuate misingi na weledi wa kazi hiyo.

“Kitakachotukosanisha naye ni kama atakandamiza uhuru wa habari,” alisema Nanai.

“Tunampongeza waziri mpya, Dk Harrison Mwakyembe kwa kuteuliwa na pia tunampongeza Nape Nnauye anayeondoka kwa kazi kubwa aliyoifanya. Kuondoka kwake kumetushtua kwa sababu tulikuwa naye kwenye kazi na sasa itabidi tuanze na mtu mpya.”

Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi alisema Nape ameondoka kishujaa kwa sababu alikuwa amebeba matumaini ya Taifa.

Alisema kutokana na kuondoka kishujaa, anayo nafasi ya kuteuliwa tena kuongoza wizara nyingine na alimsifu kwa jinsi alivyosimamia suala la kuvamiwa kwa studio za Clouds Media.

Mhadhiri wa Sayansi ya Siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Mohamed Bakari alisema kitendo cha kuondolewa kwa Nape saa chache baada ya kupokea ripoti, kinaashiria kuwa Rais John Magufuli hapendi kushauriwa.

“Waziri aliyewekwa, Dk Harrison Mwakyembe ameonyesha kutosimamia mambo yake katika wizara alizotoka. Hana msimamo,” alisema Dk Bakari na kuongeza kuwa ni mapema kumzungumzia waziri mpya wa Katiba, Profesa Kabudi kwa kuwa ndio kwanza ameteuliwa.

Askofu Gwajima

Askofu Josephat Gwajima, ambaye alisema habari iliyomtuhumu kuwa amezaa na mwanamke mmoja wa jijini Dar es Salaam ndiyo iliyosababisha Clouds kuvamiwa, jana pia alijibebesha mzigo wa Nape.

Akiwa katika ziara ya kituo cha redio cha EFM, Askofu Gwajima alisema: “Sababu zilizofanya Nape aenguliwe zinanihusu sana mimi, sababu mkuu wa mkoa alivamia mahali kuwalazimisha warushe kipindi kinachonihusu. “Nataka kila mtu ajiulize je, ni nani aliyekwenda kushinikiza Clouds kwamba material (kipindi) za kumchafua Askofu Gwajima zipigwe, ni nani? Nani alikuwa nyuma ya Mkuu wa Mkoa hata kiasi kwamba Nape aondolewe uwaziri?”

Wanamuziki wazungumza

Nape pia alikuwa anaongoza wizara inayowahusu wasanii, ambao pia wameeleza kushtushwa.

“Nape endelea kuwa mwerevu,” alisema mwanamuziki wa miondoko ya Bongo Fleva, Nick wa Pili alipozungumza na gazeti hili.

Nick alisema inauma ingawa haijulikani kwa nini amebadilishwa na kuwekwa mwingine, lakini kitendo cha kuondolewa kwake ni pengo kwa wasanii kwa sababu alikuwa ni mtu anayepatikana kirahisi.

“Tusubiri tuone huyu mpya itakuwaje. Inawezekana akaendeleza mazuri tuliyoanza Nape,” alisema Nick wa Pili.

Rais wa Mfuko wa Muziki Tanzania, Dk Donald Kisanga alimtaka Nape kusonga mbele.

“Mapambano bado yanaendelea. Wewe bado kijana tena jasiri, bado una fursa ya kufanya vitu vingi zaidi,” alisema.

Alisema kinachosikitisha ni kuondolewa kwenye nafasi aliyopo kwa sababu alionekana kuimudu, ingawa matumaini yapo pia kwa anayekuja.

Muigizaji aliyebobea, Dk Cheni alisema hakuna anayefahamu Rais anawaza nini, hivyo ni vyema kusubiri kitakachotokea.

Mwigizaji mwingine wa filamu, Johari Chagula alisema uamuzi huo umemuuma kwa sababu Nape alikuwa waziri pekee aliyejitokeza hadharani na kupigana vita moja, akisikiliza matatizo ya wasanii bila kupitia mtu mwingine.

“Kiukweli alitutoa eneo moja kutupeleka jingine. Alikuwa amesimama katikati ya masilahi yetu,” alisema Johari.

Mstuko kwa wanamichezo

Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Wavu Tanzania (Tava), Agapa Agostino alisema ni mapema Nape kuondolewa kwa kuwa tayari alikuwa na mikakati mingi katika kuboresha tasnia ambayo ameiachia njiani.

“Naheshimu uteuzi wa Rais. Ni maamuzi yake, lakini naona kama imekuwa mapema mno Nape kuondolewa. Pamoja na yote, namshauri mrithi wake kuendeleza mipango yote mizuri iliyoachwa na Nape na mabaya kuyaweka kando,” alisema.

Kocha wa judo, Zaid Hamis alisema misimamo ya Nape katika kutetea masuala ya habari ndiyo imechangia kuenguliwa katika nafasi hiyo.

Katibu Mkuu wa Chama cha Riadha Arusha, Alfredo Shahanga alisema mwenye uamuzi ni Rais, na kwamba watafanya kazi na yeyote yule watakayeletewa.

“Rais ndiye mwenye mamlaka ya kuteua mawaziri hivyo maadamu kaona inafaa Nape aondoke ni sawa na sisi tutafanya kazi na waziri yeyote tutakayeletewa,” alisema.