Pembe za ndovu 52,522 zakamatwa kwa majangili

Muktasari:

Kaimu Mkurugenzi Kitengo cha Kuzuia Ujangili wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Robert Manda amesema hayo jana alipokuwa akitoa taarifa ya namna wanavyohifadhi pembe hizo mbele ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii.

Dar es Salaam. Imeelezwa kuwa pembe za ndovu zilizotokana na ujangili nchini ni 52,522 wakati zile zilizopatikana kutokana na vifo vya asili ni 31,556.

Kaimu Mkurugenzi Kitengo cha Kuzuia Ujangili wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Robert Manda amesema hayo jana alipokuwa akitoa taarifa ya namna wanavyohifadhi pembe hizo mbele ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii.

Manda amesema pembe hizo zimehifadhiwa katika maghala matatu likiwamo la Dar es Salaam ambako ni makao makuu, Ngorongoro na jingine lililo chini ya Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa).

Amesema katika pembe hizo, kuna moja ya mwaka 1960 yenye uzito wa kilo 86.

Mbali ya idadi hiyo ya meno ya ndovu waliouawa kwa uharamia kuwa mengi zaidi wale waliokufa kwa njia njia za kawaida, Kaimu Mkurugenzi, Huduma za Ulinzi wa Wanyamapori wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (Tawa), Faustine Masalu amesema matukio ya ujangili yamepungua ikilinganishwa na miaka iliyopita.