Profesa Ndalichako: JPM ana imani na wanawake

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako

Muktasari:

  • Profesa Joyce Ndalichako alikuwa akifungua kongamano la kimataifa la wanawake likijadili nafasi yao katika Malengo Endelevu ya Maendeleo (SDG).

Dar es Salaam. Serikali imechukua hatua kadhaa kuhakikisha kwamba wanawake wanapata nafasi kwenye vyombo vya maamuzi, baadhi yake ikiwa ni kuwapa nafasi za uongozi katika ngazi za juu serikalini.

Hayo yamesemwa leo Machi 8, jijini Dar es Salaam na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako wakati akifungua kongamano la kimataifa la wanawake likijadili nafasi yao katika Malengo Endelevu ya Maendeleo (SDG).

Profesa Ndalichako amesema Rais John Magufuli ana imani na utendaji wa wanawake ndio maana amewateua kwenye wizara nyeti kama vile elimu, afya na madini akiamini kwamba watafanya kazi kikamilifu kuleta maendeleo ya nchi.

Amesema Serikali imejidhatiti kutekeleza malengo yote 17 ya maendeleo endelevu ikiwamo kuleta usawa wa kijinsia na kuleta kutoa fursa ya elimu hasa kwa mtoto wa kike.

"Serikali tunajitahidi kutekeleza malengo ya maendeleo hasa lengo la nne la elimu. Tumeshuhudia ongezeko la wanafunzi wanaoandikishwa kupitia sera ya elimu bure. Pia, tumeboresha mafunzo ya walimu na kuweka uwiano wa mwalimu na mwanafunzi darasani," amesema.

Amesema Serikali inasisitiza elimu kwa watoto wa kike kwa sababu wananyimwa fursa ya kwenda shule ili kujikomboa kifikra, pia kupata fursa ya ajira kuwawezesha kumudu maisha yao.

"Tunafanya jitihada kuboresha elimu hapa nchini. Tunaangalia pia elimu ya juu, tunashirikiana na wadau mbalimbali katika kuboresha mfumo wa elimu hapa nchini," amesema Profesa Ndalichako.

Awali, akizungumzia nafasi ya mwanamke kwenye elimu, Balozi wa Ufaransa nchini, Frederic Clavier amesema nchi yake inashirikiana na Serikali kuhakikisha kwamba wanaboresha masomo ya sayansi kwa shule za sekondari na vyuo vikuu hapa nchini.

Amesema siku chache zijazo, timu ya wanafunzi wa elimu ya juu kutoka Ufaransa watafika hapa nchini kujifunza na kubadilishana uzoefu na wanafunzi wa vyuo mbalimbali vya hapa nchini.

"Tutaendelea kushirikiana na serikali ya Tanzania katika elimu. Lakini pia Tanzania inatakiwa kuhamasisha umahiri wa lugha zaidi ya moja, nchi mbili za jirani (Rwanda na Burundi) zinatumia kifaransa, itapendeza Tanzania ikiweka mkazo kwenye lugha hiyo," amesema Clavier.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Taaluma za Sayansi Tanzania (Taas), Profesa Esther Mwaikambo amesema idadi finyu ya wanawake wanashiriki katika maeneo ya utafiti na maendeleo, uchapaji, uongozi serikalini na sekta binafsi.

Ameongeza kuwa sababu za wanawake kukosa fursa katika nyanja za  sayansi, teknolojia na uvumbuzi zinaanzia katika ukosefu wa fursa ya elimu na uwiano katika uwekezaji, mazingira ya kazi yasiyo rafiki, imani za kitamaduni na mila potofu.

"Kila mahali duniani lazima kushirikisha wanawake katika maamuzi ili maendeleo yawe fanisi na endelevu. Hili litakamilika kwa kubadilisha mtazamo wa jamii, kuleta uhuru na usawa wa kijinsia, kuamua ukubwa wa familia," amesema Profesa Mwaikambo.