Rais Angola awafukuza mkuu wa polisi, usalama jeshini

Muktasari:

Lourenço amemfuta kazi Kamanda Mkuu wa Jeshi la Polisi Ambrósio de Lemos na nafasi yake imechukuliwa na Alfredo Mingas. Pia alimwondoa António José Maria katika nafasi ya mkuu wa usalama wa taifa jeshi na nafasi yake imechukuliwa na Apolinário José Pereira.

Makamanda walioondolewa waliteuliwa na mtangulizi wake José Eduardo dos Santos na walikuwa wakionekana kuwa ni watiifu kwa kiongozi huyo.

 

Luanda, Angola. Rais Joao Lourenco amewafukuza kazi kamanda wa jeshi la polisi pamoja na mkuu wa upelelezi katika mabadiliko makubwa ya kwanza ya vyombo vya usalama tangu alipoingia madarakani Septemba mwaka huu.

Lourenço amemfuta kazi Kamanda Mkuu wa Jeshi la Polisi Ambrósio de Lemos na nafasi yake imechukuliwa na Alfredo Mingas. Pia alimwondoa António José Maria katika nafasi ya mkuu wa usalama wa taifa jeshi na nafasi yake imechukuliwa na Apolinário José Pereira.

Makamanda walioondolewa waliteuliwa na mtangulizi wake José Eduardo dos Santos na walikuwa wakionekana kuwa ni watiifu kwa kiongozi huyo.

Lourenco aliyechukua nafasi ya kiongozi wa muda mrefu dos Santos, amekuwa akichukua hatua ambazo wadadisi wa siasa wanasema anadhihirisha mamlaka makubwa aliyonayo katika koloni hilo la zamani la Ureno.

Hivi karibuni alifunga chombo cha habari kilichoanzishwa na dos Santos. Grecima kwa kiasi kikubwa kilitajwa kuwa taasisi ya propaganda iliyoanzishwa na dos Santos. Shughuli zake zilirejeshwa kwenye kitengo cha mawasiliano ya ikulu.

Hatua kubwa zaidi ilikuwa ya kumwondoa mkuu wa shirika la taifa la mafuta la Sonangol, Isabel dos Santos, binti wa dos Santos na mwanamke tajiri zaidi barani Afrika.