Ripoti ya makinikia yaibua uozo wa mikataba ya madini

Muktasari:

  • Ripoti hiyo ilitanguliwa na ripoti ya kwanza iliyokabidhiwa Mei 21 kwa Rais Magufuli ikieleza upungufu katika mapato ya madini.
  • Akiwasilisha ripoti hiyo jana, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Profesa Nehemiah Osoro alisema kampuni hiyo haikuwahi kuandikishwa Tanzania.

Dar es Salaam. Kamati ya pili iliyoundwa na Rais John Magufuli kuchunguza masuala ya kiuchumi na kisheria kwenye makinikia iliyotolewa jana imeibua uozo uliopo kwenye mikataba ya madini, huku ikifichua kutosajiliwa kwa kampuni ya Acacia Mining inayojinasibisha kuwa mmiliki wa kampuni za Bulyanhulu Gold Mines, North Mara Gold Mine na Pangea Minerals.

Ripoti hiyo ilitanguliwa na ripoti ya kwanza iliyokabidhiwa Mei 21 kwa Rais Magufuli ikieleza upungufu katika mapato ya madini.

Akiwasilisha ripoti hiyo jana, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Profesa Nehemiah Osoro alisema kampuni hiyo haikuwahi kuandikishwa Tanzania.

“Kamati imebaini na kuthibitisha kwa mujibu wa nyaraka na maelezo kutoka ofisi ya msajili wa makampuni (Brela) kuwa kampuni ya Acacia Mining Plc haikusajiliwa nchini Tanzania na wala haina hati ya utambuzi kwa mujibu wa Sheria ya Makampuni, Sura ya 212,” alisema Profesa Osoro.

Alisema kamati yake pia imebaini kampuni hiyo haikuwahi kuwasilisha nyaraka wala taarifa yoyote kuonyesha kuwa ni mmiliki wa kampuni zinazomiliki wala kuwa na hisa katika kampuni hizo.

“Kwa kuwa Acacia Mining Plc haina usajili wala utambuzi wa kisheria nchini Tanzania, haina sifa ya kupata leseni, kuchimba wala kufanya biashara ya madini nchini Tanzania. Hivyo basi, kamati imebaini kuwa Acacia Mining Plc, inafanya biashara ya madini hapa nchini kinyume cha sheria za nchi,” alisema.

Kuhusu biashara ya uuzaji na usafirisaji wa makinikia nje ya nchi, Profesa Osoro alisema uuzwaji wake umekuwa ukifanyika kwa udanyanyifu Bulyanhulu Gold Mines Ltd na Pangea Minerals Ltd.

“Jumla ya thamani ya madini katika makontena 44,077 yaliyosafirishwa nje ya nchi katika kipindi cha mwaka 1998 hadi 2017 kwa kutumia kiwango cha wastani cha Sh132.56 trilioni au Sh229.9 trilioni kwa kiwango cha juu,” alisema Profesa Osoro.

Kuhusu thamani ya madini yaliyomo kwenye makinikia katika makontena 61,320 yaliyosafirishwa nje ya nchi katika kipindi cha kati ya 1998 na 2017 kwa kutumia kiwango cha wastani ni Sh183.597 trilioni.

“Jumla ya thamani ya madini katika makontena 61,320 yaliyosafirishwa nje ya nchi katika kipindi kati ya 1998 na 2017, kwa kutumia kiwango cha juu ni Sh380.499 trilioni,” alisema.

Aliongeza kuwa jumla ya mapato ya Serikali ambayo ilipoteza ni Sh68.59 trilioni ambazo ni sawa na bajeti ya miaka miwili ya Serikali kwa kigezo cha makadirio ya mwaka 2017/2018. “Robo ya fedha hizo zingetosha kujenga reli ya standard gauge kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza,” alisema Profesa Osoro.

Kiasi cha mapato ambacho Tanzania imepoteza (kiwango cha juu) ni Sh108.46 trilioni ambazo ni sawa na bajeti inayokaribia miaka mitatu ya Serikali kwa kigezo cha makadirio ya matumizi ya mwaka 2017/2018 na gharama ya kujenga reli ya standard gauge kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza.

Kuhusu uchenjuaji wa makinikia nje ya nchi, Profesa Osoro alisema kamati hiyo ilisoma mikataba ya mauzo kati ya kampuni za uchimbaji na wachenjuaji na kugundua kuwa Serikali siyo sehemu ya mikataba hiyo, licha ya kuwapo na salio la kodi katika makinikia hayo. “Kwa msingi huo, taarifa ambazo zimekuwa zikiwasilishwa kwa TMAA (Wakala wa Ukaguzi wa Madini) baada ya kuomba taarifa hizo kutoka makampuni ya madini hazina ukweli na hazibebi takwimu sahihi kuhusu aina, kiasi na thamani ya madini yaliyochenjuliwa ambazo zingewezesha TRA kutoza kodi stahiki,” alisema Profesa Osoro.