Siku za wafuja mali CCM zahesabika

Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli.

Muktasari:

Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli amewatangazia vita watendaji ndani ya chama hicho wanaotumia mali za chama kwa masilahi yao binafsi.

Dodoma. Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli amewatangazia vita watendaji ndani ya chama hicho wanaotumia mali za chama kwa masilahi yao binafsi.

Dk Magufuli alisema hayo jana alipozungumza na watumishi wa chama hicho katika ukumbi wa makao makuu ya chama hicho maarufu kama White House akiwataka kuzitema mali hizo kwa sababu kwao itakuwa ni bahati mbaya kuchaguliwa kushika nafasi hiyo.

Vyanzo mbalimbali kutoka ndani ya mkutano huo vilisema Dk Magufuli alisema lengo la kikao hicho ambacho ni watumishi pekee walioruhusiwa kuingia, lilikuwa kujitambulisha na kuwashukuru kwa kazi waliyofanya wakati wa uchaguzi.

“CCM ni chama kikubwa chenye mali na rasilimali nyingi, lakini inashangaza kuona wanachama wake au chama chenyewe kinakuwa ombaomba, katika uongozi wangu siwezi kukubaliana na jambo hilo hata kidogo,” chanzo kilimnukuu Dk Magufuli.