TRL, Rahco kuvunjwa

Muktasari:

Serikali itaunda Shirika la Reli Tanzania (TRC) ili kuboresha huduma za reli nchini.

Bunge limepitisha Muswada wa Sheria ya Reli ya mwaka 2017 ambayo itaanzisha shirika jipya la reli.

Shirika hilo litaundwa baada ya kuvunjwa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) na Kampuni Hodhi ya Mali za Reli (Rahco).

Muswada huo uliopitishwa leo Jumatano  bungeni uliwasilishwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa.

Akiwasilisha muswada huo, Profesa Mbarawa amesema shirika jipya litajulikana

Shirika la Reli Tanzania (TRC) ambalo litakuwa na majukumu ya kusimamia, kuendeleza miundombinu ya reli na kutoa huduma ya usafiri. Amesema watumishi waliokuwa chini ya TRL ni 1,900 na 38 wa Rahco.

Akiwasilisha maoni, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu, Moshi Kakoso amesema wanaishauri Serikali kuweka utaratibu mzuri kwa mwananchi kupata

haki zao yanapotokea matatizo ya kufutwa na kuchelewa kwa safari za gari moshi.

“Shirika la reli limekuwa likifuta safari au kuchelewa kwa gari moshi pasipokujali haki za abiria,” amesema Kakoso.

Ameshauri Serikali kuweka utaratibu mzuri, wa wazi na wa haki utakaotumika kuhamisha wafanyakazi kwenda kwenye shirika jipya au wengine kwenda ofisi zingine za Serikali.

Kamati imeshauri bomoabomoa kwenye

maeneo ya shirika la reli iendelee isipokuwa wananchi waliomilikishwa

walipwe fidia.

Kambi ya Upinzani Bungeni imeshauri muda wa kuwarejeshea nauli abiria baada ya gari moshi kuchelewa uwe ni saa sita badala ya saa 24 ili kuwafanya watendaji wa shirika kuwajibika.

Akisoma maoni kwa niaba ya msemaji wa kambi hiyo, Mbunge wa Moshi Mjini (Chadema), Jaffar Michael amesema kama Serikali itaona ni vyema muda ukabaki uleule, basi angalau kuwe na jukumu la shirika kuwapatia abiria waliocheleweshwa chakula na malazi ili kuwapunguzia usumbufu.

Kuhusu faini kwa abiria, Michael amesema wanashangazwa na matakwa ya kifungu cha 47(2) kumtoza abiria asilimia 100 ya nauli pale anapopanda bila kuwa na tiketi.

“Ni ukweli usiopingika kuwa abiria wengi wanatoka maeneo ya mbali na njia ya reli, hivyo wanaweza kujikuta hawajakata tiketi ya safari au mara kadhaa ofisi za kutolea tiketi huwa zinakuwa na foleni na pengine

abiria huwa na dharura,” amesema.

Ameshauri anayepanda gari moshi bila kuwa na tiketi angalau atozwe faini ya asilimia 50 ya zaidi ya nauli iliyotakiwa kutozwa.

Wabunge wakichangia muswada huo wamesema wakati wa kuvunjwa kwa TRL na Rahco, masilahi ya wafanyakazi yazingatiwe na kuhakikisha wanaobomolewa nyumba zao kupisha ujenzi wanalipwa

haki zao.

Mbunge wa Nzega Mjini (CCM), Hussein Bashe amesema kaya zipatazo 500 zinatakiwa kuhama kupisha ujenzi wa reli jimboni kwake na wapo ambao wameishi maeneo hayo kwa zaidi ya miaka 80

Mbunge wa Igalula (CCM), Mussa Ntimizi alihoji kampuni ya reli ilikuwa wapi hadi wakawaacha watu kujenga ndani ya hifadhi ya reli.

Akizungumzia fidia, Profesa Mbarawa amesema mwananchi anayevamia barabara

hawezi kulipwa fidia bali kama barabara imemfuata huyo atalipwa.