Video yawakamatisha 10 Rorya

Kamanda wa mkoa wa kipolisi wa Tarime/Rorya, Andrew Satta

Muktasari:

Habari zinasema idadi ya waliokamatwa na Jeshi la Polisi mkoani Mara kuhusiana na tukio hilo imefikia 10 baada ya kusambaa mitandaoni.

Rorya. Video ya tukio la mwanamke akicharazwa bakora imesaidia kunaswa kwa watu waliokuwa wakimpiga mwanamama huyo.

Habari zinasema idadi ya waliokamatwa na Jeshi la Polisi mkoani Mara kuhusiana na tukio hilo imefikia 10 baada ya kusambaa mitandaoni.

Video ya juzi inaonyesha wavulana tofauti wakimcharaza viboko kwa zamu mwanamke aliyelala chini, mithili ya mwanafunzi anayeadhibiwa na walimu wake baada ya kufanya makosa.

Kamanda wa mkoa wa kipolisi wa Tarime/Rorya, Andrew Satta amesema mwanamke huyo alipigwa viboko na watu sita ambao waliamrishwa na wajumbe wa baraza la mila la kabila la Wasimbiti (Irienyi ndodo).“Inadaiwa kuwa mhanga alikuwa akilalamikiwa na mama yake na aliamua apelekwe katika baraza hilo baada ya kumtuhumu mama yake kuwa ni mchawi,” amesema Kamanda Satta.

Kamanda amesema polisi tayari wanawashikilia watuhumiwa 10 kuhusiana na tukio hilo na watano kati yao ni viongozi wa baraza la mila, akiwemo mwenyekiti na wajumbe wake wanne.