Vigogo watano Chadema washindwa kuripoti polisi

Muktasari:

Vikao vya Kamati ya Kudumu za Bunge vilivyoanza leo mjini Dodoma vimetajwa kuwa chanzo cha viongozi hao kutofika polisi


Dar es Salaam. Viongozi watano wa Chadema waliotakiwa kuripoti leo Jumanne Machi 13, 2018 Kituo Kikuu cha Polisi jijini Dar es Salaam, wameshindwa kufika kutokana na kuanza kwa vikao vya Kamati ya Kudumu ya Bunge, vilivyoanza leo.

Viongozi walioshindwa kufika leo ni mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ambaye pia ni mbunge wa Hai; naibu katibu mkuu (Bara) na mbunge wa Kibamba, John Mnyika; mbunge wa Kawe na mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Halima Mdee; Esther Matiko (Tarime Mjini) na John Heche wa Tarime Vijijini.

Wakili wa vigogo hao, Alex Massaba ameiieleza MCL Digital leo kuwa viongozi hao wameshindwa kufika kutokana na kwenda mjini Dodoma kuhudhuria vikao vya kamati.

"Kama unavyojua kati ya viongozi walioitwa watano ni wabunge na kwa sasa vikao vya kamati vimeanza hivyo wanapaswa kuwepo na kushiriki shughuli za kibunge,” amesema Massaba.

"Kati ya hao Mashinji (katibu mkuu) na Mwalimu (naibu katibu mkuu-Zanzibar) sio wabunge ndio maana wamefika kuitikia wito na tunasubiri kupewa maekekezo.”