Wabunge waliosimamishwa waweka mikakati

Muktasari:

  • Wabunge watano kati ya hao waliopigiwa simu wamesisitiza kwamba wataendelea kubainisha jinsi bajeti iliyotengwa na Serikali wakati wanasimamishwa ilivyo na changamoto za utekelezwaji wake.

Dar es Salaam. Wabunge wanane waliokuwa wamesimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge kwa muda na makosa tofauti wanatarajiwa kurejea kwenye chombo hicho cha kutunga sheria mwisho wa mwezi huu baada ya kumaliza kutumikia adhabu zao huku baadhi yao wakiahidi kuendeleza moto wa bajeti.

Wabunge watano kati ya hao waliopigiwa simu wamesisitiza kwamba wataendelea kubainisha jinsi bajeti iliyotengwa na Serikali wakati wanasimamishwa ilivyo na changamoto za utekelezwaji wake.

Mei, 2016 Bunge kupitia Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ilipitisha azimio la kuwasimamisha kuhudhuria vikao vya Bunge baadhi ya wabunge wa Kambi ya Upinzani waliodaiwa kufanya vitendo vya vurugu ndani ya ukumbi na kudharau mamlaka ya Spika Januari, 27, 2016.

Wabunge hao ni Zitto Kabwe (Kigoma Mjini), John Heche (Tarime), Halima Mdee (Kawe), Tundu Lissu (Singida Mashariki), Pauline Gekul (Babati), Godbless Lema (Arusha Mjini) na Ester Bulaya (Bunda) ambao adhabu yao ilitokana na kitendo chao cha kupinga msimamo wa Spika kuhusu Bunge kuonyeshwa ‘live’.