Wataka makaburi ya ghorofa

Muktasari:

Walisema baadhi ya maeneo ambayo mila na desturi za watu wake haziruhusu kuchoma maiti, wameanza kutumia mtindo huo ambao katika kaburi moja wanaweza kuzikwa watu 10 hadi 15.

Dar es Salaam. Baadhi ya wasomi, viongozi wa dini na wadau wa mazingira wameshauri kuanzishwa utaratibu wa kaburi moja kuzikwa watu wengi wa familia au ukoo ‘ghorofa’, ili kukabilia na changamoto ya kujaa kwa maeneo ya kuzikia badala ya kuchoma.

Walisema baadhi ya maeneo ambayo mila na desturi za watu wake haziruhusu kuchoma maiti, wameanza kutumia mtindo huo ambao katika kaburi moja wanaweza kuzikwa watu 10 hadi 15.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Iringa, Jimson Sanga alisema siyo rahisi watu kukubali kuchoma moto maiti za ndugu zao kutokana na imani kutoruhusu.

Mdau wa Mazingira wa Asasi isiyo ya Serikali ya Tunsilime ya jijini Dar es Salaam, Dk John Palagyo alisema kutokana na ongezeko kubwa la watu, lazima maeneo ya maziko yajae.

“Tangu awali, ilikuwa lazima kutafuta suluhisho la tatizo hili, kama makaburi yamejaa njia pekee iliyobaki ni kutenga maeneo mapya, koo au familia zifundishwe namna ya kutumia mfumo wa kuzika watu wengi kwa nyakati tofauti kwenye kaburi moja,” alisema.

Askofu wa Kanisa la Pentekoste Shalom la Tabata jijini Dar es Salaam, Charles Msellah alisema hakuna haja ya kuanza kuhangaika na maeneo ya maziko kwa sasa, wakati kuna mapori mengi yanayoweza kutumika kuzikia.

Mufti wa Tanzania, Sheikh Mkuu Abubakar Zubeir alisema utaratibu wa makaburi mengi ya Kiislamu kutojengewa unatoa nafasi kwa watu kutumia tena kaburi lililokaa muda mrefu.