Watanzania, wageni wadaiwa kushirikiana matukio ya ugaidi

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yusuf Masauni (wapili kutoka kushoto), Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Idara ya Polisi ambaye pia ni Naibu Mkuu wa Polisi nchini (DIGP), Abdulrahman Kaniki (wapili kutoka kulia), Kamishna wa Fedha wa jeshi hilo, Albert Nyamhanga (kushoto) na Katibu wa Baraza hilo, Merise Mwanyema wakiimba wimbo wa mshikamano daima kabla ya kufungua Kikao cha baraza hilo kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Magereza Ukonga, jijini Dar es Salaam jana. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Muktasari:

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni ameyasema hayo wakati akifungua kikao cha saba cha Baraza la Utekelezaji la Wafanyakazi wa Idara ya Polisi.

Dar es Salaam. Ushirikiano mbaya kati ya baadhi ya Watanzania na wageni wenye nia mbaya umeibua sintofahamu inayosababisha viwapo viashiria vya ugaidi hapa nchini.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni ameyasema hayo wakati akifungua kikao cha saba cha Baraza la Utekelezaji la Wafanyakazi wa Idara ya Polisi.

“Upo uwezekano mkubwa wanaotekeleza uhalifu huo wanapitia katika mafunzo yasiyo rasmi ndani na nje ya nchi na yanahusisha matumizi ya silaha na mbinu mbalimbali za kisayansi zinazowasaidia kutekeleza uhalifu huo,” amesema

Masauni amesema zipo kambi zinazotumika kama maficho ya siri yanayowawezesha watu hao kutekeleza uovu na imeshuhudiwa kuibuka kwa matukio mbalimbali yenye viashiria hivyo ikiwamo kuvamiwa kwa vituo vya polisi.

“Lazima tuimarishe mikakati yetu ya kukabiliana na matukio haya ya kidhalimu kwa maslahi na ustawi wa watu wetu na Taifa na tunataka muafaka wa kubaini kusambaratisha na kuondoa mitandao inayojihusisha na matukio ya aina hii bila ya kuionea haya wala huruma,”amesema.

Mwenyekiti wa wa baraza hilo, Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, Abdulrahman Kaniki amesema wanakabiliwa na  changamoto ya ufinyu wa bajeti ambao unasababisha utekelezaji wa majukumu yao kuwa mgumu .

“Hizi changamoto tunazileta rasmi baada ya maazimio ya Baraza la Utekelezaji la Wafanyakazi wa Idara ya Polisi tutakapofikiana,”amesema Kaniki.