Wawakilishi wapitisha marekebisho ya Katiba ya Zanzibar

Rais wa Zanzibar,Dk  All Mohamed Shein

Muktasari:

Mabadiliko hayo yatajulikana kama Sheria ya Marekebisho ya 11 ya Katiba ya Zanzibar ya 2016.

Zanzibar. Baraza la Wawakilishi (BLW) limepitisha marekebisho ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 yanayompa uwezo Rais kuteua wajumbe wawili bila kushauriana na Kiongozi wa Upinzani ambaye kwa sasa hayupo katika baraza hilo.

Mabadiliko hayo yatajulikana kama Sheria ya Marekebisho ya 11 ya Katiba ya Zanzibar ya 2016.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Haroun Ali Suleiman amesema vifungu viwili vilihitaji kufanyiwa marekebisho kufuta maneno ya vyama na kiongozi wa upinzani.

Miongoni mwa vifungu vilivyorekebishwa ni cha 66 kinachoondolewa maneno ‘vyenye uwakilishi ndani ya baraza la wawakilishi’ na ‘iwapo hakuna kiongozi wa upinzani’

Waziri amesema madhumuni ya mabadiliko hayo ni kutoa fursa ya uteuzi pale ambako hakuna kiongozi wa shughuli za upinzani ndani ya Baraza la Wawakilishi.

Amesema masharti ya kifungu cha 66 hayatoi uwezo na mamlaka kwa Rais kufanya uteuzi kwa kuwa yanamlazimisha kushauriana ama na kiongozi wa upinzani au vyama vya siasa vyenye uwakilishi ndani ya BLW.