Timu mpya zitakazoleta upinzani Ligi Kuu Bara

Muktasari:

Timu hizo zilimaliza kwenye nafasi mbili za juu za makundi mawili (Kundi A na B) katika mechi za Ligi Daraja la Kwanza kwani kila kundi lilitakiwa kutoa timu mbili zitakazopanda daraja.

Hatimaye wiki moja iliyopita Mwadui ya Shinyanga ilitwaa ubingwa wa Ligi Daraja la Kwanza na kuzipiku timu nyingine tatu zilizofanikiwa kupanda ligi msimu ujao. Timu zingine zilizorejea Ligi Kuu ni African Sports ya Tanga, Majimaji FC ya Songea na Toto Africans ya Mwanza.

Timu hizo zilimaliza kwenye nafasi mbili za juu za makundi mawili (Kundi A na B) katika mechi za Ligi Daraja la Kwanza kwani kila kundi lilitakiwa kutoa timu mbili zitakazopanda daraja.

Kwa upande wa Kundi A, African Sport na Majimaji zilifuzu wakati kwenye Kundi B zilifuzu timu za Mwadui FC na Toto Africans.

Timu hizo zinazomilikiwa na wakazi wa maeneo timu zinapotokea, siyo ngeni kwenye Ligi Kuu kwani kwa miaka ya nyuma timu zote zilishawahi kushiriki Ligi Kuu kabla ya kushuka. Hivi sasa timu hizo zinatarajiwa kutoa upinzani mkubwa kwenye Ligi ikiwamo kuwania ubingwa wa ligi. Timu hizo ziko kama ifuatavyo:

Majimaji FC ‘Wanalizombe’

Ni miongoni mwa timu ambazo zilikuwa tishio nchini katika miaka ya 1980 hadi iliposhuka daraja mwaka 2000. Kisha ikarejea tena mwaka 2009 na kushuka mwaka 2010. Mashabiki wengi wa soka nchini wanaikumbuka Maji Maji ya Songea maarufu kwa jina la Wanalizombe.

Maji Maji ambayo ilianzishwa mwaka 1977 ilipata umaarufu mkubwa mwaka 1980, mwaka ambao timu hiyo ilipata nafasi ya kushiriki kwa mara ya kwanza Ligi Daraja la Kwanza ambayo kwa sasa ni Ligi Kuu.

Uwezo wa timu hiyo

Kocha Mkuu wa Majimaji, Hassan Banyai anasema, “Mafanikio ya timu yangu yalitokana na kufanya kazi kwa umoja, nilishirikiana na wachezaji, pia umoja uliokuwapo kati ya viongozi, benchi la ufundi, wafadhili na mashabiki ulitufanya twende vizuri na tufanikiwe.”

Mipango kwenye Ligi Kuu

Kocha wa Majimaji, Banyai anasema kuwa ndoto zake kwa timu hiyo ni kuchukua ubingwa wa ligi ndani ya muda mfupi. “Tuliwahi kuchukua ubingwa wa Muungano miaka ya nyuma, hivi sasa tunataka kurudisha heshima yetu ya hapo awali kwa kuchukua ubingwa mapema,” alisema kocha huyo.

African Sport ‘Wanakimanumanu’

Hii ni moja ya timu ambazo ziliwahi kufanya vizuri miaka ya nyuma na kujiwekea heshima. Mpinzani wake mkubwa ni Coastal Union iliyopo Ligi Kuu. African Sport iliwahi kutwaa ubingwa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania huku ikitamba kati ya miaka ya 80 na 90.

Ilitwaa kombe hilo mwaka 1988, lakini ikateremka daraja miaka mitatu baadaye, mwaka 1991.

Kocha Mkuu wa timu hiyo, Joseph Lazaro ambaye ni beki wa kushoto wa zamani wa Coastal Union na Yanga anasema katika mpango wao wa kutengeneza timu mpya amepanga kuongeza wachezaji saba tu kwenye usajili.

“Tuna imani kubwa na uwezo wa hawa vijana wetu, yatakuwapo maboresho kidogo tu, Tunajua Ligi Kuu ina ugumu wake, kikubwa kwetu kitakuwa ni maandalizi ya mapema,” anasema.

Nguvu ya timu yake

Kocha wa timu hiyo, Joseph Lazaro anasema kuwa kilichowabeba zaidi ni umri mdogo wa wachezaji ambao uliwawezesha kucheza vizuri. Pia ushirikiano na nidhamu ya mazoezi.

“Pia tulijiandaa vyema kwa kufanya zaidi mazoezi na kucheza kama timu,” anasema Lazaro.

Uongozi ulivyojipanga

Katibu Mkuu wa timu hiyo, Khatibu Enzi anasema,”Tunataka kurudisha historia ya nyuma kwa kupanda ligi na kuchukua ubingwa kama tulivyofanya mwaka 1988, hakuna kinachoshindikana kwetu. Tuna nguvu na umoja katika timu yetu, ugumu ulikuwa kupanda, lakini sasa tumefika.”

Toto Africans ‘Wanakishamapanda’

Toto Africans imepanda Ligi Kuu baada ya juhudi za muda mrefu. Klabu hiyo ilishuka daraja kutokana na ukata ulioikabili mwaka 2013. Kabla ya kushuka daraja miaka miwili iliyopita, Toto ilikuwa imecheza misimu sita mfululizo kwani ilikuwapo kwenye ligi tangu msimu wa 2007/08. Hivi sasa timu inaongeza utamu wa soka kwa Kanda ya Ziwa baada ya Kagera Sugar, Stand United na Mwadui nao kuwa na nafasi kwenye ligi.

Nguvu za timu hiyo

Kocha Mkuu wa Toto, John Tegete anasema, “ Kilichotubeba kupanda Ligi Kuu ni usajili mzuri, licha ya umaskini wa timu yetu tulitafuta wachezaji bora wenye viwango na uzoefu mzuri.”

Mipango kwenye ligi

Kocha Tegete anasema watafanya marekebisho kwenye nafasi mbalimbali ili kuhakikisha ligi ya msimu ujao wanafanya vyema na kuleta ushindani.

Mwadui FC

Kifedha wako vizuri na wako chini ya udhamini wa mgodi wa almasi wa Petra Diamonds -Wiliamson uliopo Mwadui Shinyanga. Timu hii ilitamba msimu uliopita kwenye Ligi Daraka la Kwanza, lakini ikashindwa kwa pointi mbele ya majirani zao Stand United.

Mwadui FC ni moja ya timu kongwe nchini, Ilicheza Ligi kuu kati ya miaka ya 70 na kisha kushuka kwenye miaka ya 80.

Moja ya mafanikio ya timu hiyo ni kufika nusu fainali ya kusaka ubingwa wa Tanzania kwa kuitoa Yanga kwa mikwaju ya penalti.

Nguvu ya timu

Kocha Mkuu wa Mwadui FC, Jamhuri Kiwhelo ‘Julio’ anasema, “ Timu yangu ilikuwa bora kwenye idara zote hasa kwenye idara ya ushambuliaji kwani ilifunga mabao mengi zaidi kuliko timu zingine zilizocheza na sisi.

“Usajili wa wachezaji wazoefu kama Athumani Iddi ‘Chuji’, Uhuru Selemani, Razack Khalfani uliisaidia timu, kimsingi usajili ndiyo uliochangia Mwadui kupanda Ligi Kuu,” anasema Julio.

Mipango kwenye Ligi

Kocha Julio anasema,”Mimi na timu yangu tumekuja kusaka ubingwa wa Ligi Kuu na kama siyo hivyo basi nikichemka sana niwe kwenye nafasi ya tatu.