Imani za kishirikina zinavyotesa mastaa Ulaya

LONDON, ENGLAND. DUNIA ina mambo unaambiwa. Kiungo wa Arsenal, Matteo Guendouzi amedai kwamba washambuliaji Alexandre Lacazette na Pierre-Emerick Aubameyang kila siku asubuhi wanakwenda kumgusa bega la kushoto ili wawe na bahati.

Kiungo huyo wa Arsenal alisema pacha hao kwenye fowadi amekuwa akiishi nao kama kaka zake tangu alipojiunga na timu hiyo akitokea Lorient, Julai 2018.

Hilo linalofanywa na Aubameyang na Lacazette kumgusa bega la kushoto Guendouzi wakiamini watakuwa na bahati ni ushirikina unaofanya mastaa wengi kwenye soka la Ulaya.

Kwa Afrika, suala la ushirikina michezoni ni la kawaida tofauti na Ulaya. Kuna mastaa wakubwa kabisa wamekuwa wakiamini kwamba wanapofanya tukio fulani kabla ya mechi basi litawafanya kuwa na bahati kwenye mchezo huo au kwa siku hiyo.

Mastaa hawa hapa wamekuwa na mambo ya kishirikina kabla ya kuingia uwanjani kuzitumikia timu zao huko Ulaya.

Cristiano Ronaldo

Staa wa Juventus katika kitu ambacho anakimini kwamba anapokifanya kimekuwa kikimletea bahati basi ni kuhakikisha anakuwa peke yake kwenye korido wakati anaelekea uwanjani. Anapofika uwanjani, Ronaldo ni lazima atangulize mguu wa kulia kwanza kabla ya kutazama juu.

John Terry

Beki huyo wa zamani wa Chelsea na England, kitu ambacho alikuwa akikiamini ni kuketi kwenye siti ileile ndani ya beki mar azote timu yake inapokwenda kucheza mechi. Terry, pia hata muziki aliyokuwa akisikiliza ni albamu ya Usher tu na hata gari lake alikuwa akiegesha sehemu moja tu na kikingaugoko chake kilikuwa kimoja tu kwa misimu yote.

Phil Jones

Vitu ambavyo amekuwa akivifanya beki Phil Jones inategemea kama timu yake ya Manchester United inacheza ugenini au nyumbani. Kwenye hilo ndio ataamua ni soksi ya mguu gani aanze kuvaa kabla ya kuingia uwanjani. Mguu ambao anakuwa wa kwanza kuvaa soksi kwenye mechi za nyumbani, basi hauwezi kuwa huo huo kwenye mechi za ugenini.

Jermain Defoe

Straika, Jermain Defoe naye amekuwa na mambo yake anayoamini yasiyotofautiana na ushirikina. Fowadi huyo amekuwa akihakikisha kwamba katika kila mechi kabla hajaingia uwanjani kucheza basi ni lazima anyoe nywele, akimini kwamba kucheza mechi akiwa na nywele ndefu kunamsababisha majeruhi.

Gareth Bale

Shida kubwa inayomsumbua Gareth Bale na kushindwa kufurahia maisha yake ya soka ni majeruhi ya mara kwa mara. Kutokana na hilo, staa huyo wa kimataifa wa Wales amekuwa na kawaida ya kutoboa matundu soksi zake kila anapoingia uwanjani akiamini kwamba kwa kumfanya hivyo kunamfanya asipate majeruhi hasa maumivu ya misuli ya kigimbi.