Wanasoka waliopiga watu kwa ulevi watoka gerezani

Muktasari:

Wanasoka hao ambao wamekaa gerezani kwa takriban mwaka mmoja walimshambulia dereva wa mtangazaji wa televisheni na maofisa wa serikali wakati wakiwa wamelewa.

Wanasoka wa Russia, Pavel Mamaev na Alexander Kokorin leo wameruhusiwa kutoka gerezani baada ya kukaa jela kwa karibu mwaka mmoja kutokana na kupatikana na hatia ya kushambulia usiku wakati wakiwa wamelewa.
Televisheni ya serikali ilimuonyesha kiungo wa Krasnodar, Mamaev, 31, na mshambuliaji wa Zenit Saint Petersburg,Kokorin, 28, wakiondoka gereza ambako wamekuwa wakitumikia kifungo lililoko katika mji wa Belgorod ulio kusini magharibi.
Shirika la habari la Russia liliripoti kuwa Zenit Saint Petersburg imeshasaini mkataba mpya na Kokorin.
"Tuliamua kusaini mkataba na Kokorin ambao unaenda hadi mwisho wa msimu," mkurugenzi mkuu wa klabu hiyo, Alexander Medvedev aliliambia shirika la habari la RIA Novosti. Msimu wa soka unaisha mwezi Mei.
Wakiwa wamevalia fulana zenye kofia, wawili hao walikimbilia kwenye gari huku wakikataa kujibu maswali ya waandishi wa habari waliokuwa wamekusanyika nje ya gereza.
Mwezi huu mahakama iliruhusu wawili hao watoke gerezaniu mapema baada ya kupatikana na hatia ya kushambulia mwezi Mei mwaka jana jijini Moscow.
Ukijumlishwa na muda waliokaa mahabusu kabla ya kesi, wanasoka hao wamekaa gerezani kwa miezi 11 katika hukumu yao ya kifungo cha miezi 17/18 jela.
Katika usiku uliokuwa wa kinywaji Oktoba mwaka jana, Mamaev na Kokorin kwanza walimshambulia dereva wa mtangazaji wa televisheni wakati akisubiri katika maegesho ya magari.
Katika shambulio hilo lililorekodiwa kwenye video, baadaye wawili hao wakawashambulia maofisa wa serikali, wakimpiga mmoja wao kwa kiti.