Afisa habari wa zamani Simba afariki dunia

Dar es Salaam. Aliyekuwa afisa habari wa Simba SC na mwandishi wa habari za michezo, Asha Muhaji amefariki dunia mchana wa leo, Jumatano.

Asha (50) amekutwa na mauti wakati anaendelea na matibabu hospitali ya Hindu Mandali iliyopo jijini Dar es Salaam.

Mdogo wa marehemu, Habibu Kaumo alithibitisha kifo cha dada yake kuwa kilitokana na kusumbulia na TB ya ngozi iliyogundulika baada ya kufanyiwa vipimo juzi Jumanne.

Alisema kuwa marehemu mara kadhaa alikuwa akiumwa, lakini tatizo hilo halikugundulika hadi alipopelekwa katika hospitali hiyo ambako alilazwa tangu Alhamisi ya wiki iliyopita.

"Alikuwa anaumwa na mwili wake ulikuwa ukidhoofika kadri siku zinavyokwenda bila kujua tatizo kuwa ni TB ya ngozi ambayo awali haikujulikana kama anayo," alisema na kuongeza

"Baada ya vipimo ndipo amegundulika kuwa ana tatizo hilo lakini akiwa katika hali mbaya sana ya kupumulia mashine, madaktari wamejitahidi kadri ya uwezo wake, lakini Mungu ameamua kumpumzisha mchana wa leo." alisema

Habibu alisema msiba upo nyumbani kwa wazazi wake Mabatini, Kijitonyama ambapo mazishi yatafanyika leo Alhamisi kwenye makaburi Mwinyimkuu yaliyopo Magomeni, Dar es Salaam.

"Tumeutoa mwili hospitalini na kwenda kuuhifadhi msikiti wa Mahmuru uliopo Upanga ambapo kesho leo atafanyiwa ibada kabla ya kuelekea makaburi kumpumzisha, marehemu hajaacha mtoto" alisema

Asha enzi za uhai wake aliwahi kufanyakazi kwenye vyombo mbalimbali vya habari ikiwemo Uhuru na New Habari akiwa mhariri wa michezo gazeti la Rai.