Hii ndio sababu Manula kuwaweka benchi makipa Simba

Muktasari:

  • Simba inajiandaa na mchezo wa hatua ya makundi Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya AS Vita ya Congo.

Dar es Salaam. Unajua kwa nini mlinda mlango wa Simba,  Aishi Manula anapata nafasi ya kucheza mechi za Ligi Kuu Bara na za kimataifa?  Sasa huu ndiyo ukweli.

Aishi ambaye amecheza mechi zote za Ligi Kuu kasoro michezo miwili miwili, ambayo walidaka wengine.

Mlinda mlango huyo aliyesajiliwa na Simba msimu uliopita, alikosa mechi na KMC akadaka Deogratius Munishi 'Dida' na hakumaliza mechi ya Mbeya City aliumia akaingia Ally Salim.

Kocha wa makipa, Mohammed Mwarami amesema, Aishi ataendelea kudaka kwa sababu hajafanya makosa.

"Hata kwenye mataifa wanayojua soka mfano Manchester United kipa anayejulikana ni De Gea, licha ya timu hiyo kuwa maarufu, wengi hawamjui mlinda mlango wa pili, "alisema Mwarami aliyekuwa mlinda mlango wa zamani wa Simba.

Amesema, nafasi ya kipa ni ya kipekee,  hivyo huwezi kumchezesha kila mlinda mlango.

"Kipa anatakiwa kukaa langoni akijiamini, sasa ikitokea amepumzishwa anaporudi anacheza kwa  hofu akiogopa kuharibu, "alisema Mwarami.

Amesema, hilo ni tatizo ambalo linaweza kusababisha akafungwa zaidi kwa sababu ya kukosa kujiamini.

Simba imefanya mazoezi yao ya mwisho leo Jumatano asubuhi kwenye Uwanja wa Boko Veterani.