Makonda awashangaa wanaowabeza nyota wa Stars

Muktasari:

  • Taifa Stars ilipoteza 2-0 dhidi ya Senegal ndipo wadau mbalimbali waliibuka na kuanza kuponda viwango vya wachezaji.

Dar es Salaam. Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amejikuta akishindwa kuzuia hisia zake juu ya wadau mbalimbali wanaowabeza wachezaji wa timu ya Taifa Tanzania 'Taifa Stars'.

Akizungumza katika ufunguzi wa Mradi wa Gesi, Kigamboni, Makonda alisema ameshangaa wadau mbalimbali wakiwazungumzia vibaya wachezaji baada ya kupoteza mbele ya Senegal.

"Nimeumizwa na matokeo ya Taifa Stars, lakini nimeumizwa zaidi kwa watu kuwabeza wachezaji wetu ambao wametubeba watanzania ambao ndani ya miaka 30, haikuwezekana lakini wao wamepambana mpaka tupo Afcon leo hii," alisema.

Makonda alisema alizungumza na wachezaji hao pamoja na nahodha Mbwana Samatta na wamemuhakikishia kwamba watafanya vizuri katika mchezo wao dhidi ya Kenya.

"Sisi Afrika Mashariki tunajuana vizuri kwahiyo Mhesimiwa Rais wala usiwe na wasiwasi tutafanya vizuri katika mchezo huu ambao tunahitaji ushindi na wachezaji wapo vizuri," alisema Makonda.

Aliongeza iwapo Mh Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli aweze kutoa neno lolote la kuwapa moyo kuelekea katika mchezo ujao.

Tanzania itacheza na Kenya Alhamisi mchezo utakaopigwa saa kumi na moja jioni.