Manchester United yajitosa kwa Mandzukic kuzipa pengo la Lukaku

Muktasari:

  • Zikiwa zimebaki saa chache kabla ya kufungwa kwa dirisha la usajili nchini England, Manchester United wako mbioni kumsajili Mario Mandzukic kuziba pengo la Romelu Lukaku.

Manchester United wamerudi mezani kufanya mazungumzo Juventus kwa ajili ya kupata huduma ya mshambuliaji, Mario Mandzukic baada ya Romelu Lukaku kutimkia Inter Milan ya Italia.

Lukaku alitua leo asubuhi nchini Italia tayari kufanyiwa vipimo kabla ya kujiunga na Inter Milan kwa uhamisho wa Paund 73 millioni.

Mandzukic ambaye hii sio mara yake ya kwanza kuhitajika na Manchester United, anatazamwa kama mchezaji anayeweza kuziba pengo la Lukaku Old Trafford.

Pia, Manchester United wanahusishwa na kuiwania saini ya mshambuliaji wa Athletic Bilbao, Inaki Williams kama chaguo lingine endapo juhudi za kumng'oa Mandzukic nchini Italia zitagonga mwamba.

Kwa mujibu wa mwandishi wa Sky Sports nchini Italia, anluca Di Marzio alisema dili la Mandzukic kujiunga na Manchester United linaweza kukamilika kabla ya kufungwa kwa dirisha la usajili England.

Mandzukic ambaye ni Mcroatia, aliwahi kuzichezea Bayern Munich na Atlético Madrid kabla ya kujiunga na kibibi kizee cha Turin, Julai mosi ya miaka minne iliyopita (2015).