Miraji awapigia hesabu Chama, Kanda

Muktasari:

  • Miraji Athuman katika michezo minne iliyocheza Simba amefanikiwa kufunga mabao matatu akiwa nyuma ya Meddie Kagere mwenye mabao sita.

Dar es Salaam. Winga wa Simba, Miraji Athuman amesema uwepo wa wachezaji wenye uzoefu katika namba anayocheza kunamsaidia kuongeza bidii, ili kuepuka kusugua benchi kwa msimu huu.
Kocha wa Simba, Patrick Aussems amekuwa akiwatumia zaidi kiungo Clatous Chama ama Deo Kanda, wakati Miraji akimtumia kama mchezaji wa akiba, isipokuwa katika mechi dhidi ya Biashara United alicheza dakika 90.
Hilo linamfanya Miraj kuongeza juhudi mazoezini na kila anapopewa nafasi katika kuhakikisha anamshawishi kocha wake kumpa namba katika kikosi cha kwanza.
"Kwanza nacheza na watu wenye uzoefu mkubwa na wenye vipaji vya juu, hilo linanifanya mimi niendelee kupambana kila kunapoitwa leo ili kocha nisimuangushe anaponipa nafasi ya kucheza,"
"Simba ni timu inayohitaji ushindi na malengo yao yapo tofauti na timu ambazo nimetoka, huku wanafikiria ubingwa tu, lazima nipambane kwa bidii ili kufikia ndoto ya kuwa miongoni mwa wachezaji wenye msaada ndani ya klabu," alisema Miraj.