Ndayiragije: Lazima tuweke heshima nyumbani

Muktasari:

Stars inahitaji ushindi katika mchezo wa Jumapili au suluhu katika mchezo huo wa mkondo wa awali wa ili kusonga mbele kwenye harakati za kufuzu kucheza kombe la dunia baadae mwaka 2022 nchini Qatar.

WAKATI timu ya Taifa 'Taifa Stars' ikihitaji ushindi wowote ili kusonga mbele katika harakati za kuwania nafasi ya kufuzu kucheza Kombe la Dunia, Kaimu Kocha mkuu wa timu hiyo, Etienne Ndayiragije amesema wana kila sababu ya kuifunga Burundi keshokutwa Jumapili.
Stars itarudiana na Burundi kwenye uwanja wa Taifa Dar es Salaam baada ya sare ya bao 1-1 mjini Bujumbura Burundi Jumatano iliyopita.
Akizungumzia mchezo wa marudiano, kocha huyo raia wa Burundi alisema una kila sababu ya Stars kushinda nyumbani.
"Niliwahi kusema kufuzu kushiriki Kombe la Dunia ni hatua nyingine, lakini kufanya vizuri katika harakati za kufuzu ni suala jingine pia, tunachokihitaji ni kufanya vizuri katika harakati hizi," alisema kocha huyo.
Alisema amekuwa akiwasoma wapinzani wao mara kwa mara kabla na baada ya mchezo wao wa awali, wanatambua ubora na udhaifu wa kikosi cha Burundi, hivyo atayatumia kuhakikisha Stars inafanya vizuri.