Simba yaondoka mchana huu kufuata kombe lao Morogoro

Muktasari:

Simba ilikuwa ikabidhiwe kombe lake Jumamosi iliyopita, lakini kupata udhuru kwa mgeni rasmi kulikwamisha sherehe hizo za ubingwa kutofanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Mabingwa wateule wa Ligi Kuu Bara, Simba itaondoka mchana huu kwenda Morogoro tayari kwa mchezo wao wa mwisho utakaochezwa kesho dhidi ya Mtibwa Sugar na kukabidhiwa ubingwa wao kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.

Ikumbukwe katika mchezo wa mzunguko wa kwanza uliochezwa Uwanja wa Uhuru, Simba ilishinda mabao 3-0, yaliyofungwa na nahodha John Bocco, Clatous Chama na Emmanuel Okwi.

Meneja wa Simba, Patrick Rweyemamu alisema watakutana mchana kambini kabla ya kuanza safari ya kuelekea Morogoro.

"Wanatakiwa kuondoka wachezaji wote, benchi la ufundi na baadhi ya viongozi, lakini kama kutakuwa na mchezaji ambaye atashindwa kuwa sehemu ya safari ya kuelekea Morogoro nitafahamu tukiwa tumeanza safari yetu," alisema Rweyemamu.

Simba imechukua ubingwa kwa mara ya pili mfululizo na inakuwa mara ya 20, kwake kutwaa ubingwa huo wakati watani zao Yanga wao ndio mabingwa wa kihistoria wamelitwaa taji hilo mara 27.