TFF yamtupia virago Amunike

Muktasari:

Amunike aliingoza Taifa Stars kufuzu kwa mara ya kwanza kwa Fainali za Afconi baada ya miaka 39.

Dar es Salaam. Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limethibisha kuachana na kocha timu ya taifa 'Taifa Stars', Emmanuel Amunike kwa makubaliano ya baina ya pande mbili.

Uamuzi wa TFF umekuja wakati kukiwa na presha kubwa ya wadau wa soka nchini wakishindikiza Amunike hatimuliwe tangu Tanzania ilipofuzu kwa mara ya kwanza kwa Afcon Aprili na baada ya mashindano hayo yanayoendelea Misri.

Katika mashindano ya Afcon2019, Tanzania ikiwa Kundi C pamoja na Algeria, Senegal na Kenya ilipoteza mechi zote na kuambulia pointi tatu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Shirikisho hilo kupitia kwa Ofisa Habari wake, Cliford Ndimbo imesema shirikisho na kocha wamefikia makubaliano ya kusitisha mkataba baina yao.

Alisema shirikisho litatangaza kocha wa muda ambaye atakiongoza kikosi cha timu ya taifa kinachotarajia kushiriki mashindano ya Kombe la Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN).

"Makocha wa muda watatangazwa baada ya kamati ya dharura ya kamati ya utendaji (Emergency Committee) itakayofanyika Julai 11 mwaka huu," ilisema taarifa ya Ndimbo na kuongeza kuwa mchakato wa kutafuta kocha mpya umeshaanza.

Amunike aliingia mkataba wa miaka miwili wa kuiona Tanzania Agosti 6, 2018 akichukua nafasi ya Salum Mayanga aliyekuwa anakaimu nafasi hiyo.