Waziri Mwakyembe aitabiria makubwa Kilimanjaro Stars

Muktasari:

Timu za taifa za Tanzania Bara 'Kilimanjaro Stars' na Zanzibar 'Zanzibar Heroes' zimepangwa Kundi C pamoja na Kenya na Djibout.

Dar es Salaam.Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe anaamini Kilimanjaro Stars itakwenda kufanya maajabu Uganda katika mashindano ya Kombe la Chalenji.

Mashindano hayo yataanza Desemba 7, timu za taifa za Tanzania Bara 'Kilimanjaro Stars' na Zanzibar 'Zanzibar Heroes' zimepangwa kukutana katika mchezo wa ufunguzi wa kundi C.

Mechi hiyo itachezwa Jumapili saa 10 jioni jijini Jinja mara baada ya kumalizika kwa mchezo wa kwanza wa kundi hilo baina ya Kenya na Djibout ambao utachezwa kuanzia saa 8.30 mchana.

Akizungumza katika mazoezi ya Kilimanjaro Stars, Mwakyembe amesema anapoona wachezaji wanavyojituma katika mazoezi ndio itakuwa silaha ya kufanya vyema.

Mwakyembe ameshuhudia mazoezi hayo yanayoendelea Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam yanayosimamiwa na kocha Etienne Ndayiragije, Juma Mgunda pamoja na wasaidizi wao Seleman Matola na Zuber Katwila.

"Tanzania kwa sasa tupo juu na tunaheshimika ingawa tukikutana na timu inajiandaa zaidi tunarudi tulipotoka,"

"Kikubwa wachezaji wajitume wajiamini na kujua nyuma kuna kundi la Watanzania ambao linawategemea wafanya kitu cha tofauti.

"Watanzania pia waiunge mkono timu yao kwani sapoti yao ni muhimu zaidi kuwapa moyo wachezaji wasijione wapo wenyewe,"amesema Mwakyembe.