Zana Coulibaly na umaarufu Simba, Yanga

Muktasari:

Zana Coulibaly ni miongoni mwa wachezaji wa Simba walio jijini Arusha tayari kwa mchezo wao wa Ligi Kuu Bara utakaopigwa kesho Jumanne Uwanja wa Sheikh Amri Said.

Dar es Salaam. Mbali na ubora wao wa uwanjani kwa wachezaji wa Simba  beki wao wa kulia, Muivory Coast Zana Oumar Coulibaly amepata umaarufu mkubwa kwa mashabiki nje ya uwanja.

Wadau wa soka wanajua Simba ina wachezaji wengi wenye sifa za uwanjani kama, Mnyarwanda Meddie Kagere, Mzambia Cletous Chama na wengine lakini anapotajwa Zana tu watu lazima wafurahi.

Beki huyo ambaye staili yake ya nywele amezibadili kwa kuziweka brichi, mbali na uwezo wa kucheza nafasi ya beki wa kulia anamudu pia kucheza kushoto na kati.

Tangu asajiliwa kwenye dirisha dogo mwaka huu amekuwa maarufu na kutajwa midomoni mwa washabiki wa timu zote Simba, Yanga na timu nyingine. 

Si kwa sababu kiwango chake tu lakini amekuwa mchangamfu nje ya uwanja na burudani kwa watu wengi lakini pia video tofauti ambazo zimekuwa zikimwonyesha akicheza muziki na kuwachekesha wachezaji wenzake kama kukatika mauno na kurembua zimemfanya apendwe zaidi.