VIDEO: Miss Tanzania akaa siku sita bila kuoga

Muktasari:

Miss Tanzania2018 amejikuta akikaa siku sita bila kuoga wakati akipanda mlima Kilimanjaro kutokana na baridi kali iliyopo katika mlima huo.

Dar es Salaam. Unapomzungumzia Miss ni mtu mmoja mrembo na msafi wakati wowote.

Hata hivyo, jambo la kuwa msafi kwa Miss Tanzania 2018, Elizabeth Makune katika siku sita alizokuwa akipanda Mlima Kilimanjaro lilikuwa ngumu kwake.

Miss Tanzania huyo alilazimika kukaa siku sita bila kuoga alipokuwa akishiriki kampeni ya ‘Twenzetu Kileleni’ iliyoandaliwa na Waziri wa Maliasili na Utalii nchini Tanzania, Dk Hamis Kigwangallah na kuwashirikisha wadau mbalimbali wa utalii wakiwemo wasanii.

Elizabeth ambaye alikuwa mmoja wa watu waliofanikiwa kufika kilele cha mlima huo aliiambia Mwananchi katika moja ya mambo ambayo yatabaki kumbukumbu maishani mwake ni kushindwa kuoga kwa siku sita.

“Nikiwa Dar es Salaam naweza kuoga hata mara nne kwa siku, lakini baridi la Mlima Kilimanjaro asikuambie mtu bana, nilijikuta nakata siku sita bila kuoga,” amesema.

Hata hivyo, amesema changamoto alizokutana nazo wakati wa kupanda mlima huo zimemfundisha vitu vikubwa katika maisha ikiwemo kutokubali kukata tamaa mapema.

“Katika safari hii kuna baadhi yetu waliishia njiani, lakini mimi nilijipa moyo kuwa lazima nitoboe,  licha ya kuwa kuna wakati ilifika nikakata tamaa kutokana na kukutana na vilima vikali vilivyojaa barafu,” amesema.

Wakati wa kurudi na kupanda mlima huo, mrembo huyo amesema atafanya hivyo baada ya kufanya mazoezi ya muda mrefu ya kutembea,  kwa kuwa moja ya sababu ya kuchoka ni kutokuwa na mazoezi hayo ya kutosha