Hallelujah ya Diamond yavunja rekodi

Muktasari:

Wimbo uliowahi kutazamwa na watu wengi ndani ya muda mfupi nchini.

Video ya wimbo mpya wa mwanamuziki Diamond Platnumz, Hallelujah umefikisha watembeleaji milioni moja ndani ya saa 16 tangu ulipowekwa katika chaneli ya Youtube na kuwa wimbo uliowahi kutazamwa na watu wengi ndani ya muda mfupi nchini.

Wimbo Hallelujah uliowekwa saa sita usiku, unaivunja rekodi iliyowekwa mwezi ulipita na Seduce Me wa Alikiba ambao ulifikisha watembeleaji milioni moja ndani ya saa 37 uliowekwa katika mtandao wa Vevo. Diamond katika wimbo huo amewashirikisha wasanii wa Jamaica, Morgan Heritage.

Hallelujah ulifikisha watembeleaji milioni moja ilipofika saa kumi jioni.

Muda mchache kabla ya kufikisha watazamaji milioni moja Diamond aliwashukuru mashabiki wake kwa kuupokea vizuri wimbo huo.

“Nawashukuru kwa kuniunga mkono, tuzidi kusonga mbele ili dunia ione uwezo wa mtoto wa Kitanzania, “ aliandika katika mtandao wa Instagram.