Diwani mbaroni Dodoma

Muktasari:

Polisi wakiri kumshikilia, kamanda wa polisi wa mkoa agoma kuzungumzia tuhuma zinazomkabili, meya wa jiji asema kukamatwa kwake kuna uhusiano na masuala ya ardhi

Dodoma. Diwani wa Makole (CCM), jijini hapa Habel Shauri anashikiliwa na polisi kwa tuhuma ambazo hazikuwekwa wazi na polisi, lakini zikihusha masuala ya ardhi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto alisema jana kwamba “Ni kweli tumemkamata tunachunguza. Hatuwezi kulizungumza kwenye vyombo vya habari tutakujulisha siku tutakayompeleka mahakamani na ndipo utakapojua kilichosababisha akamatwe.”

Alipoulizwa ni siku ya ngapi tangu wamkamte diwani huyo Muroto alisema “Hatuwezi kusema ni siku ya ngapi kubwa uchunguzi unaendelea.”

Wakati Kamanda Muroto akisema sababu za kumkamata zitawekwa wazi atakapofikishwa mahakamani, Meya wa Jiji la Dodoma, Profesa Davis Mwamfupe alisema diwani huyo anashikiliwa kuhusiana na masuala ya ardhi.

Hata hivyo, hakutaka kuingia undani wa suala hilo akisema jeshi la polisi lipo kwenye uchunguzi.

“Ni kweli amekamatwa kwa sababu ya masuala ya ardhi na bado suala hilo chini ya upelelezi. Ni mapema kusema muda tangu akamatwe, lakini nafikiri ni siku ya tano kama sio ya sita,” alisema Profesa Mwamfupe.