Mwanafunzi afanya mtihani dakika 30 baada ya kujifungua

Muktasari:

  • Awali, alijua atafanya mtihani kabla ya kujifungua lakini ilishindikana baada ya mitihani kuhairishwa.

Ethiopia. Mwanafunzi wa shule ya sekondari nchini Ethiopia mwenye umri wa miaka 21 amefanya mtihani yake ya mwisho dakika 30 baada ya kujifungua.

Mwanafunzi huyo aliyefahamika kwa jina la Almaz Derese, ambaye anatokea eneo la Metu Kaskazini mwa Ethiopia alijifungua mtoto wa kiume katika hospitali ya Metu nchini humo.

Kwa mujibu wa mwanafunzi huyo, awali alifikiri ataweza kufanya mitihani hiyo kabla ya kujifungua lakini ilishindikana baada ya mitihani kuhairishwa kwa sababu ya mfungo wa Ramadhani.

“Nilikwenda kujifungua siku ya Jumatatu muda mfupi kabla ya mtihani wa kwanza kuanza,” Almaz aliliambia Shirika la Habari la Uingereza (BBC).

“Kwa sababu nilikuwa nawaza kuhusu mtihani wangu, sikupata shida katika kujifungua”.

Akiwa katika hospitali hiyo, Almaz alifanya mitihani ya masomo matatu ikiwamo ya Kiingereza, Amharic na Hisabati na kuwa na matumaini kwamba iliyobaki atafanya shuleni baada ya siku mbili.

Mwanafunzi huyo alisema “kusoma ukiwa mjamzito si tatizo na sikutaka kusubiri kuhitimu mwaka ujayo.”