Bashiru aitaja Arusha, Chemba kwa migogoro

Muktasari:

Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amewaonya viongozi wasio na mahusiano mema baina yao na viongozi wengine kuwa hatua dhidi yao zitachukuliwa

Dodoma. Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amemuondoa katibu wa CCM wilaya ya Chemba mkoani Dodoma kutokana na mahusiano mabaya ya viongozi katika wilaya hiyo.

Amesema hayo leo Jumamosi Machi 23, 2019 wakati akizindua mkakati wa kukomaza demokrasia kwenye mashina ulioandaliwa na CCM mkoa wa Dodoma.

Amesema mbunge (wa Chemba- Juma Nkamia), mkuu wa wilaya ( Simon Odunga) na mbunge hawana mahusiano mazuri katika wilaya hiyo.

"Namuondoa katibu wangu ameshindwa kumudu kujiongeza. Nitapeleka katibu mpya pale," amesema.

Amesema matatizo kama hayo yapo wilaya za Siha, Kyela, Arusha hasa kwa mkuu wa mkoa wa Arusha (Mrisho Gambo).

Amesema kwa upande wa mkoa wa Dar es Salaam, umetulia kama mtungi wa maji.

Pia ametoa onyo kwa waziri mmoja kijana (hakumtaja jina) kuwa hana adabu amekuwa akiwatolea maneno yasiyofaa walio chini yake.

"Yeye kateuliwa na Rais na wao wameteuliwa na Rais. kujenga mahusiano ni kazi," amesema.