Kabudi aeleza sababu Tanzania kupiga hatua

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba Kabudi

Muktasari:

  • Profesa Kabudi alisema hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi mjini Unguja jana alipofika kujitambulisha baada ya kuteuliwa na Rais John Magufuli kushika wadhifa huo.

Unguja. Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba Kabudi amesema Tanzania imefanikiwa kuwa taifa linaloendelea kutokana na misingi imara iliyowekwa na waasisi wake.

Alisema yapo makabila mengi Tanzania, lakini muungano wa sauti moja inayozungumzwa na wananchi wake ni mfano wa kuigwa na mataifa mengine duniani.

Profesa Kabudi alisema hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi mjini Unguja jana alipofika kujitambulisha baada ya kuteuliwa na Rais John Magufuli kushika wadhifa huo.

“Yapo mataifa mengi yaliyowahi kuunganisha nchi zao akitolea mfano iliyokuwa Yugoslavia na sasa zimesambaratika na Senegal na Gambia kwa Afrika kutokana na kushindwa kuendeleza muungano wao,” alisema.

Naye Balozi Iddi alisema ushawishi wa uwekezaji ndani ya visiwa vya Zanzibar unapaswa kuungwa mkono na ofisi zote za kibalozi za Tanzania zilizopo mataifa mbali mbali duniani.