Lissu afunguka sifa za kugombea ubunge na urais, ajitaja mwenyewe

Muktasari:

Juni 28, 2019 Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai alitangaza kuwa Tundu Lissu amepoteza sifa za kuwa mbunge wa Singida Mashariki kupitia Chadema kwa madai hajajaza fomu za mali na madeni za viongozi wa umma pamoja na kutokutoa taarifa kwake (spika) alipo

Dar es Salaam. Aliyekuwa mnadhimu wa kambi ya upinzani bungeni nchini Tanzania, Tundu Lissu amesema licha ya Spika wa Bunge, Job Ndugai kudai hakujaza fomu za mali na madeni za viongozi wa umma bado ana sifa za kugombea nafasi yoyote ya uongozi.

Lissu aliyeko Ubelgiji kwa matibabu ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Julai 01, 2019 ikiwa ni siku chache zimepita tangu alipopoteza sifa za kuwa mbunge.

“Ili upoteze sifa ya kugombea ubunge au urais sharti uwe umekuwa na hatia, sasa mimi sijakutwa na hatia na mahakama au mahakama ya Sekretarieti ya maadili, Ndugai pekee yake hawezi kunitia hatiani bila kunisikiliza.”

“Kwa hiyo mimi naweza kugombea nafasi yoyote ya uongozi iwe ubunge au urais. Kama wanataka nisigombee wanipeleke mahakamani au kwenye mahakama ya sekretarieti na wakiniuliza kwa nini sijajaza fomu nitawaambia nitawezaje kujaza nikiwa nje ya nchi,”  amesema Lissu

Amesema fomu hizo zinapaswa kujazwa na kuziwasilisha kwa njia ya mkono lakini zinapaswa kusainiwa na wakili wa Tanzania, “Sasa mimi niko hospitalini Ubelgiji, nawezaje kuzijaza, huku nampata wapi wakili, nawezaje kuzipeleka kwa mkono? Kwa hiyo walipaswa kuniuliza kwa nini sijajaza na si kuzungumza sijajaza bila kuta sababu.”