Mbunge CUF adai akimsalimu Waziri Mpina hamjibu

Mbunge wa Mtwara Mjini (CUF), Maftah Nachuma

Muktasari:

Mbunge wa Mtwara Mjini (CUF), Maftah Nachuma amesema kila akimsalimu Waziri wa Mifugo na Uvuvi,  Luhaga Mpina hajibu salamu yake

Dodoma. Mbunge wa Mtwara Mjini (CUF), Maftah Nachuma amesema kila akimsalimu Waziri wa Mifugo na Uvuvi,  Luhaga Mpina hajibu salamu yake.

Nachuma ameibua tuhuma hizo bungeni leo Jumanne Mei 21, 2019 katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi mwaka 2019/2020.

Mbunge  huyo ametaja sababu za kutosalimiana na Waziri huyo ni kutokana na kudai kuwa anakwepa majukumu yake.

"Zaidi ya mara tatu namsalimia Waziri  hata hapo nje (ya viwanja vya Bunge) lakini hapokei salamu yangu,  tatizo ni kitu gani? Mbona Rais (John Magufuli) yupo chini kwa wanyonge lakini ninyi mnawakwepa mnaowaongoza," amesema Nachuma.

Kwa mujibu wa mbunge huyo,  chanzo cha kutokusalimiana ni Mpina kinatokana na kifo cha kijana aliyemtaja kwa jina la Abdallah Abdulrahiman aliyedai aliuawa katika mazingira tata wakati wa operesheni za uvuvi.