Mgombea DRC akimbilia mahakamani

Muktasari:

  • Kanisa Katoliki, lilisema wachunguzi wake 40,000 wa  uchaguzi walimpata mshindi tofauti kutoka matokeo rasmi  lakini kanisa hilo halikutoa maelezo  zaidi

Kinshasa, DRC. Mtihani wa matokeo ya uchaguzi bado unaiandama Jamhuri  ya  Kidemokrasia  ya Congo (DRC) baada ya mshindi wa pili Martin Fayulu kujipanga kuwasilisha  pingamizi katika Mahakama ya Katiba.

Mpinzani huyo alisema juzi kwamba atawasilisha pingamizi  mahakamani  dhidi  ya  matokeo  ya  uchaguzi  wa Rais yaliyotangaza hivi karibuni.

Muungano  wake  wa  upinzani  umesisitiza  kwamba, mgombea huyo  alipata  asilimia  61 ya kura  kwa  mujibu wa  uchunguzi wa  waangalizi  wa  Kanisa  Katoliki  lenye  ushawishi mkubwa .

Fayulu alizungumza  na wafuasi wake ambao walikusanyika  katika mji mkuu Kinshasa, kupinga  kile  walichokiita ushindi  wa wananchi ulioibiwa.

Fayulu alimtuhumu Rais  anayeondoka madarakani Joseph Kabila kwa kufanya makubaliano ya chini kwa chini na mshindi  aliyetangazwa, kiongozi  wa  upinzani  Felix Tshisekedi.

Uchunguzi  wa  Kanisa Katoliki uligundua Tshisekedi alipata  asilimia 18 ya kura, juu kidogo  ya  mgombea  wa  chama  tawala  Emmanuel  Ramazani Shadary, muungano  wa  Fayulu  ulisisitiza.

Matokeo yachapishwe

Fayulu  alitoa  wito  kwamba Tume  ya Uchaguzi (Ceni)   ichapishe matokeo, kituo  kwa  kituo.

"Wale ambao  walipanga  kuchapisha  matokeo bandia, tutapambana  nao," alisema Fayulu.

"Nitafanya kila liwezekanalo kwangu kufanya ukweli udhihiri sababu Wacongo wanataka mabadiliko," alisema.

Fayulu hata hivyo ameweka wazi kuwa kuna uwezekano mdogo wa kushinda kesi hiyo kwa sababu mahakama imeundwa na watu wa Kabila lakini alisema  hataki kuwapa kisingizio wapinzani wake kuwa hakufuata sheria.

"Tshisekedi ameteuliwa na Kabila ili kutekeleza matakwa ya utawala wa Kabila. Kabila ndiye bosi," alisema  Fayulu.

"Kabila hawezi kubaki na kusuka mpango na mtu ambaye hatakuwa na mamlaka yoyote... Tshisekedi anajijua kwamba hakushinda uchaguzi."

Fayulu alisema ana hofu kuwa kutatokea vurumai kama Ceni haitatoa takwimu sahihi za kituo kimoja kimoja cha kupigia kura na kusisitiza kuwa ni haki ya kila Mkongomani kuandamana kwa mujibu wa sheria.

Maelfu ya mashabiki wa Tshisekedi waliingia mitaani kwa furaha kusherehekea ushindi walioupata, lakini upande wa pili wafuasi wa Fayulu walijitokeza  kupinga matokeo hayo.

Matukio ya ghasia yaliripotiwa katika eneo la Kikwit, ambapo polisi wawili na raia wawili wanasemakana kuuawa.

Kuna ripoti pia mamia ya wanafunzi wamekuwa wakipinga matokeo hayo kwa kuandamana na kutimuliwa na mabomu ya machozi katika mji wa Mbandaka.

Maandamano pia yameripotiwa katika eneo la Kisangani, lakini Kusini ambapo Tshisekedi anaungwa mkono kwa wingi kumekuwa na sherehe.

Raia wa Congo  wanakabiliwa na hali isiyo ya kawaida ya  uchaguzi unaodaiwa kuwa umechakachuliwa kuelekea  upinzani  baada  ya mgombea aliyependelewa na Kabila , Shadary , kufanya vibaya katika uchaguzi.

Tume  ya Uchaguzi mapema Alhamisi ilitangaza kwamba Tshisekedi  alishinda  kwa  asilimia  38  ya  kura  wakati  Fayulu  alipata asilimia  34.

Wakati  huohuo vyama  vinavyomuunga mkono Rais  anayeondoka madarakani nchini humo vimeshinda kwa wingi  katika uchaguzi uliocheleweshwa  wa Bunge, kwa  mujibu  wa  ukusanyaji  wa hesabu  uliofanywa  na Shirika la Habari la AFP.

Vyama hivyo vimevuka kiwango kwa kupata viti 250 kinachotakiwa  kuwa  na  wingi  bungeni  katika Bunge la Taifa lenye  viti 500, kwa  mujibu  wa  matokeo yaliyowekwa  pamoja  na Ceni.

Mauaji mji wa Kikwit

Watu watano wanadaiwa kufariki kufuatia maandamano ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa rais katika eneo la Magharibi la Kikwit.

Msemaji wa polisi, kanali Pierrot-Rombaut Mwanamputu alithibitisha na kudai kwamba polisi wawili pia walipoteza maisha.

Kwa mujibu wa msemaji huyo wa polisi, mitambo ya kituo cha Radio na Televisheni ya Taifa pia iliharibiwa na waandamanaji hao.