Mikopo sekta binafsi yaongezeka mwaka 2019

Muktasari:

Serikali imesema mikopo iliyotolewa kwa sekta binafsi imeongezeka kutoka asilimia 0.8 mwaka 2017 hadi asilimia 10.6 Aprili, 2019.


Dodoma. Mikopo iliyotolewa na taasisi za fedha kwenda  sekta binafsi Tanzania imeongezeka kwa asilimia 10.6 kutoka asilimia 0.8 kati ya mwaka 2018 hadi Aprili 2019.

Hayo yameelezwa bungeni leo Alhamisi, Juni 13, 2019  na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango  alipokuwa akiwasilisha taarifa ya hali ya uchumi wa Taifa  mwaka 2018 na mpango wa maendeleo wa Taifa wa mwaka 2019/20.

Dk Mpango amesema kuongezeka kwa kasi ya ukuaji wa mikopo inayoelekezwa sekta binafsi kumechangiwa na jitihada za kuboresha mazingira ya biashara na usimamizi thabiti  wa sera ya fedha.

“Kupungua kwa mikopo chechefu kwenye benki za biashara kulikotokana na matumizi ya kanzidata ya taarifa za wakopaji katika kuidhinisha mikopo. Mikopo iliyotolewa imesaidia kuanzisha na kuimarisha shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo biashara, ujenzi na kilimo.”

“Sehemu kubwa ya mikopo kwa sekta binafsi imeendelea kuelekezwa katika shughuli binafsi na kaya ambazo zilipata wastani wa asilimia 28.8 ya mikopo yote ikifuatiwa na shughuli za biashara zilizokuwa na wastani wa asilimia 18.5 na uzalishaji viwandani asilimia 11.3,” amesema Dk Mpango.