VIDEO: Mvua Arusha zaharibu miundombinu

Mvua zinazoendelea kunyesha jijini Arusha zikiwa zimesababisha msongamano jirani na soko la Kilombero asubuhi .Picha na Filbert Rweyemamu

Muktasari:

  • Mvua iliyonyesha maeneo mbalimbali jijini Arusha kuanzia jana usiku hadi leo asubuhi Aprili 30, 2019 imesababisha madhara ikiwamo kuharibu miundombinu

Arusha. Mvua zinazonyesha jijini Arusha kuanzia jana usiku hadi leo asubuhi Jumanne Aprili 30, 2019 zimesababisha madhara ikiwamo kuharibu barabara huku nyumba kadhaa zikijaa maji.

Maeneo yaliyoathiriwa na mvua ni barabara kuu ya Arusha- Moshi huku magari madogo yakizuiwa kupita katika barabara ya  Arusha-Namanga na barabara za katikati ya Jiji la Arusha.

Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) jijini Arusha, John Kalupale amesema mvua zimesababisha athari kubwa ya miundombinu.

"Barabara ya Arusha kwenda Moshi eneo la King'ori imeharibika na magari madogo tumeyazuia kwa muda lakini   barabara kadhaa zimeharibika na tayari kazi ya ukarabati imeanza,” amesema Kalupale.

Amesema maofisa wa Tanroads mkoa wa Arusha wameanza ukaguzi kutembelea barabara zote ambazo zimeathirika na mvua na watatoa taarifa baadaye.

"Tunaendelea kutembelea barabara kujua athari za mvua baadaye tutatoa taarifa rasmi,” amesema.

Pia, kamanda wa polisi mkoa wa Arusha, Jonathan Shana amefanya ziara kukagua maeneo yaliyoathirika na mvua.

Mkazi wa Arusha,  Jumanne Saidi amesema mvua imekuwa na athari maeneo ya Daraja mbili, Unga Ltd na Uswahilini ambako maji yamejaa kwenye nyumba.

"Hali siyo nzuri kunaweza kuwa na shida kubwa kama mvua zikiendelea leo,” amesema Saidi.