Mwenyekiti UWT atoa wito kwa Serikali, wanawake

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT) wa CCM, Gaudensia Kabaka

Muktasari:

  • Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT) wa CCM, Gaudensia Kabaka ameendelea na ziara yake Unguja, Zanzibar ambapo ametoa wito kwa wananchi kujituma na kujishughulisha ili kujiinua kiuchumi

Unguja. Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM, Gaudensia Kabaka amesema ipo haja ya kuweka mikakati zaidi kuboreshwa na Serikali ili kuendelea kuwahudumia wazee ambao ndio wenye mchango mkubwa ndani ya nchi.

Kabaka ameyasema hayo leo Alhamisi Machi 14, 2019 visiwani Zanzibar wakati akiendelea na ziara yake katika mkoa wa Mjini Magharib Unguja.

Amesema kinamama ndio waasisi wa Muungano uliopo leo baina ya Tanzania bara na Zanzibar lakini pia waliosukuma kufanyika kwa mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Kabaka amesema wakati umefika kwa wanawake kuwezeshwa zaidi ili wawe sehemu ya kupigania haki za kijamii sambamba na za kiuchumi.

Pamoja na hayo amewataka kinamama kutoridhika walipo badala yake wajishughulishe na shughuli mbalimbali za ujasiriamali ambazo zitawawezesha kuwakuza kiuchumi.