Polisi Moro waua watuhumiwa wanne wa ujambazi

Muktasari:

Watuhumiwa 19 wanashikiliwa kwa tuhuma mbalimbali ikiwamo unyang’anyi na mauaji

Morogoro. Polisi Mkoa wa Morogoro imewaua watu wanne wanaodaiwa ni majambazi baada ya kurushiana risasi na askari.

Pia, inawashikilia watu 19 kwa tuhuma mbalimbali ikiwamo unyang'anyi na mauaji.

Kamanda wa polisi mkoani hapa, Wilbroad Mutafungwa amesema miili ya waliouawa imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Morogoro, huku watuhumiwa 19 wakiwa wanaendelea kuhojiwa zaidi.

Mutafungwa amesema askari wa Wilaya ya Kipolisi  Ruhembe mkoani Morogoro baada ya kupata taarifa ya kuwapo matukio ya ujambazi walifanya ufuatiliaji na kupata taarifa kuwa kuna makundi ya watu wanaojihusisha mauaji na unyang'anyi.

Amesema katika tukio hilo, polisi walikamata bunduki moja aina ya Shotgun double barrow namba 107735.

Pia, Mutafungwa amewataka viongozi wa vijiji kuendelea kutumia madaftari yao kuandikisha wanaoingia katika maeneo yao.