RC Mtwara ataka wakulima wa korosho kutobweteka

Baadhi ya wakulima katika kijiji cha Mailikumi Mtwara wakipatiwa mafunzo ya matumizi sahihi ya viuatilifu yaliyoratibiwa na Bodi ya korosho kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Naliendele na TPRI.Picha na Haika Kimaro

Muktasari:

Wakulima  wa korosho wametakiwa kuacha kujibweteka na badala yake watumie wataalamu wa kilimo na viuatilifu kwa usahihi ili kuendana na kasi ya mikoa pinzania ambayo imeanza kulima zao hilo kwa kutumia mbegu za kisasa zilizofanyiwa utafiti na chuo cha Naliendele.


Mtwara. Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Gelasius Byakanwa amewataka wakulima wa korosho mkoani humo kuwatumia wataalamu wa kilimo ili kuzalisha zao hilo kwa wingi.

Akifungua mafunzo ya matumizi sahihi ya viuatilifu kwa baadhi ya wakulima wa korosho katika kijiji cha Mailikumi leo Jumatano Juni 12, 2019, Byakanwa amesema Mikoa mingine inayolima korosho inazingatia ushauri wa wataalamu.

“Tunavyojisifu kwa kilimo cha korosho kwamba ni wazalishaji wakubwa tutambue  mikoa mingine imeanza kulima zao hili. Tukiendelea kubweteka wakati wenzetu wanalima kisasa na wana matumizi sahihi ya viuatilifu tutajikuta tunakuwa nyuma katika uzalishaji.”

“Zaidi ya asilima 60 ya korosho inatoka Mtwara ikifuatiwa na Lindi na Ruvuma, mikoa mingine wana maeneo mengi ya kulima na pengine kutumia mbegu za kisasa zilizotokana na utafiti wa chuo cha Naliendele. Chonde  chonde wana Mtwara tubadilike siku za usoni takwimu zinaweza kubadilika mkajikuta nyie ni wa mwisho,” amesema Byakanwa

Kaimu mkurugenzi mkuu wa bodi ya korosho, Francis Alfred amesema “Katika tasnia ya korosho tunaangalia kuanzia uzalishaji mpaka masoko, kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita kuanzia 2017/18 uzalishaji ulipanda na kuwa tani 313,000 lakini  2018/19 uzalishaji ni tani  244,000.”