RC Mwanri amsimamisha meneja wa TRA, aagiza uchunguzi uanze

Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri

Muktasari:

  • Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Wilaya ya Igunga mkoani Tabora, John Mgeni amesimamishwa kazi na Mkuu wa mkoa huo, Aggrey Mwanri kwa tuhuma za kudai rushwa kwa mfanyabiashara.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri  amemsimamisha kazi Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wilayani Igunga John Mgeni ili kupitisha uchunguzi wa tuhuma za kudai rushwa zinazomkabili.

Mwanri alitoa amri ya kusimamishwa jana Juni 24, 2019 wakati wa semina ya uelimishaji wa wafanyabiashara kuhusu ulipaji wa kodi, iliyofanyika wilayani humo.

Kiongozi huyo wa mkoa alifikia uamuzi wa kumsimamisha kazi Mgeni baada ya mfanyabiashara mmoja kulalamikia alikutwa na kosa la kutotoa stakabadhi ya mauzo ya Sh10,000 na kutakiwa kulipa faini ya Sh4.5 milioni au kupelekwa mahakamani.

Ilidaiwa  meneja huyo alimwambia mfanyabiashara huyo anaweza kumpa Sh2 milioni ili asipelekwe mahakamani wala asilipe adhabu inayohitajika Kisheria.

Kutokana na tuhuma hizo, Mwanri aliiagiza Taasisi za Kuzuia na Kudhibiti Rushwa (Takukuru) kufanya uchunguzi na kumtaka meneja huyo kutoingia ofisini mpaka utakapokamilika.

Kwa upande Meneja wa TRA Mkoa wa Tabora, Thomas Masese aliwataka wafanyabiashara kuwa huru kufichua watendaji wa mamlaka hiyo wanaofanya kazi kinyume cha sheria.

Alisema TRA haitambughudhi mfanyabiashara yoyote ambaye atakafichua uovu wa watumishi wa TRA.