Rais Magufuli atangaza siku tatu za maombolezo

Muktasari:

Rais wa Tanzania, John Magufuli amesema bendera za nchi zitapepea nusu mlingoti kwa siku tatu kuomboleza vifo vya Watanzania 64 waliofariki katika mlipuko wa moto uliotokana na ajali ya lori lililokuwa limebeba shehena ya mafuta ya petroli kuanguka eneo la Msamvu mkoani Morogoro.


Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli ametangaza siku tatu za maombolezo kufuatia vifo vya Watanzania 64 vilivyotokana na ajali ya lori la mafuta iliyotokea jana Jumamosi eneo la Msamvu mkoani Morogoro.

Katika ajali hiyo watu 64 walifariki dunia na wengine zaidi ya 70 wakijeruhiwa ambapo wamelazwa Hospitali ya Rufaa Morogoro na wengine wakihamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dar es Salaam kwa matibabu zaidi.

Taarifa iliyotolewa jana usiku Jumamosi ya Agosti 10, 2019 na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu ya Tanzania imesema maombolezo hayo yatakwenda sambamba na bendera ya taifa hilo kupepea nusu mlingoti.

Katika taarifa hiyo imesema Rais Magufuli amemwagiza Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kwenda mkoani Morogoro kumwakilisha katika mazishi yanayotarajiwa kuanza kufanyika leo Jumapili Agosti 11, 2019.

Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi.