Spika Ndugai asema Heche ajiandae kung’oka 2020

Mbunge wa Tarime Vijijini (Chadema), John Heche

Muktasari:

Spika wa Tanzania, Job Ndugai amemtahadharisha mbunge wa Tarime Vijijini (Chadema) John Heche kwamba Sh9 bilioni zitamtoa katika uchaguzi ujao mwaka 2020

Dodoma. Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amesema kampeni za Chama cha Mapinduzi (CCM) katika jimbo la Tarime Vijijini 2020 zitakuwa ni nyepesi na John Heche mbunge wa jimbo hilo kwa sasa kupitia Chadema ajiandae.

Spika Ndugai ametoa kauli hiyo leo Jumatatu bungeni Februari 3,2019 ambapo amesema kuna ufujaji mkubwa wa miradi ya Serikali wakati mbunge wake Heche amekuwa ni mpiga kelele kwa mambo mengine.

"Kama kuna kitu kimenishangaza ni taarifa za Tarime, sisi sote ni madiwani ambao lazima tujue miradi iliyoko kwenye majimbo yetu, sasa kama mtu ameshindwa kusimamia Sh9 bilioni Tarime hivi mwakani atasema nini," amesema Ndugai.

Ndugai ambaye ni mbunge wa Kongwa amesema kiasi cha fedha hizo kama zingetolewa katika jimbo la Kongwa, asingeomba kitu kingine chochote kwa Serikali bali mambo yangekuwa mazuri.

Amesema uchaguzi wa mwakani jimbo la Tarime kutakuwa na wimbo mmoja tu wa bilioni 9 na ushindi utakuwa mapema.