Uchaguzi Serikali za Mitaa nchini Tanzania giza nene kwa vyama vya upinzani

Muktasari:

Wakati Chama cha Mapinduzi (CCM) kikieleza kupata ratiba na kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa, vyama vya upinzani vimesema vipo njia panda na havijui kinachoendelea kuhusu uchaguzi huo

Dar es Salaam. Wakati Chama cha Mapinduzi (CCM) kikieleza kupata ratiba na kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa, vyama vya upinzani vimesema vipo njia panda na havijui kinachoendelea kuhusu uchaguzi huo.

Vyama hivyo; Chadema, ACT-Wazalendo, CUF na UDP, vimesema hadi sasa havijui uchaguzi huo utafanyika lini.

Jana, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Josephat Kandege aliliambia Mwananchi kuwa uchaguzi utafanyika Novemba.

Alitaja mwezi huo baada ya kuulizwa kuhusu maandalizi ya uchaguzi huo unaofanyika kila baada ya miaka mitano, ikiwamo kanuni zake.

“Kanuni ya mwisho ilikuwa imetoka lakini ilikuwa inafanyiwa maboresho maana wadau wote walishirikishwa,” alisema.

“Tarehe bado... ninachojua uchaguzi utafanyika mwezi Novemba, na leo ni mwezi wa nane, sidhani kama unaweza kuwa miezi mitatu ya kampeni kama ulivyo uchaguzi mkuu. Kinachofanyika sasa ni hamasa kwa ajili ya uandikishaji wa Daftari wa Wapigakura,” alisema.”

Wakati Kandege akieleza hayo Katibu wa Oganaizesheni wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM, Pereira Silima alisema tayari wameshapatiwa kanuni pamoja na ratiba kuwa uchaguzi huo utafanyika Novemba 24, “tulipewa na Tamisemi pamoja na ratiba.”

Baada ya maelezo hayo, Mwananchi lilirejea tena kwake na kumweleza kuhusu maelezo hayo ya Silima na akasema, “unajua nilikuwa nje ya ofisi inawezekana wakati sipo hivyo vitu vimeshakamilika. Nipe muda nifuatilie.”

Kwa habari zaidi soma gazeti la Mwananchi la leo Jumatano Agosti 7, 2019