Vikao vya Kamati za Bunge kuanza leo

Muktasari:

Vikao vya kamati za Bunge vinaanza leo Jumanne jijini Dodoma ikiwa ni maandalizi ya mkutano wa 15 wa Bunge la Bajeti ya mwaka 2019/20 ambao utaanza Aprili 2, 2019

Dodoma. Vikao vya kamati za Bunge kwa ajili ya mkutano wa 15 wa Bunge la Bajeti ya Serikali ya mwaka 2019/2020  unaanza leo Jumanne Machi 12, 2019m huku kesho wabunge wote wakipokea mapendekezo ya Serikali ya mpango na kiwango cha ukomo wa bajeti ya mwaka huo wa fedha.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa jana Jumatatu na Ofisi ya Bunge jijini Dodoma, vikao hivyo vinaanza kuanzia leo hadi Machi 30, 2019 kabla ya kuanza kwa mkutano wa Bunge la bajeti Aprili 2, 2019.

“Wajumbe wa kamati zote watashiriki Mkutano wa Wabunge wote tarehe Machi 12, 2019 kwa ajili ya kupokea mapendekezo ya Serikali ya Mpango na kiwango cha Ukomo wa mwaka wa fedha 2019/2020,” imesema taarifa hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kesho kutwa Jumatano Machi 13,2019 kamati hizo za sekta zitaanza ziara za kutembelea na kukagua miradi mbalimbali na ziara za kufuatilia uwekezaji pamoja na thamani halisi ya matumizi ya fedha za umma.

Machi 22 hadi 24, 2019, Kamati za Sekta zitaanza uchambuzi wa taarifa za utekelezaji wa Bajeti kwa mwaka wa fedha 2018/2019 na makadirio ya matumizi kwa mwaka wa fedha 2019/2020 kwa mujibu wa Kanuni ya 98(2).

“Uchambuzi utaendelea hadi Machi 28, 2019 na Machi 29, 2019, Kamati zitakamilisha uchambuzi na kuanza maandalizi ya taarifa za kamati zitakazowasilishwa bungeni,” imesema taarifa hiyo.